Ahadi ya Uhuru ya bilioni 50 yatatua utata wa mgao wa mapato kwa kaunti

Maseneta
Maseneta
Ahadi  ya rais Uhuru Kenyatta kuongeza mgao wa pesa za kaunti hadi shilingi bilioni 50 siku ya Jumanne ulifanikisha kupata suluhu kwa utata unaozingira mfumo wa ugavu wa mapato kwa serikali za kaunti.

Katika mkutano uliyofanyika ikuli ya Nairobi, Rais Kenyatta aliwashawishi baadhi ya maseneta waliyokuwa wakipinga mfumo mpya wa ugavi wa mapato hatua ambayo imelemaza shughuli za serikali za kaunti.

"Tumekubali pendekezo hilo. Lakini tumeipa jukumu kamati ya wanachama 12 kubuni mfumo bora utakaozingatia nyongeza hiyo ya shilingi bilioni 50," Seneta wa Laikipia John Kinyua alisema.

Mkutano huo ambao ulihudhuriwa na aliyekuwa Waziri Mkuu, Raila Odinga na mwenyekiti wa Baraza la Magavana Wycliffe Oparanya, uliafikiana kwamba kulingana na jinsi hali ya uchumi itakavyokuwa katika mwaka wa kifedha wa 2020/2021, Serikali itatoa shilingi Bilioni 50 za ziada kwa kaunti katika juhudi za kuimarisha ugatuzi nchini.

Kutokana na hatua hiyo, Rais aliwahimiza Maseneta hao kusuluhisha kwa haraka utata wa ugavi wa mapato katika Bunge la Seneti ili kuzuia kuvurugwa kwa utoaji wa huduma katika kaunti.

Bunge la Seneti liliwakilishwa katika mkutano huo na Mheshimiwa Samuel Poghisio (Kiongozi wa Wengi), Mheshimiwa Irungu Kang'ata (Kiranja Mkuu), James Orengo (Kiongozi wa wachache) na Mheshimiwa Fatuma Dullo (Naibu wa wa walio wengi katika bunge hilo)

Wengine waliokuwepo ni Maseneta Beatrice Kwamboka na Johnes Mwashushe Mwaruma wa Taita Taveta.