Alifanya nini? Pata kufahamu kwa nini China inampiga Ozil vita

ozil china
ozil china

Kiungo wa Arsenal Mesut Ozil ameondoshwa kwenye mchezo wa video wa Pro Evolution Soccer (PES) 2020 toleo la Uchina baada ya kuikosoa nchi hiyo kwa kuwatesa jamii ya Waislamu ya Uighur.

Ozil, 31, ambaye ni Muislamu, amewaita Wauighur (Wachina wa asili ya Kiislamu) "mashujaa wanaokabiliana na mateso".

Pia ameukosoa utawala wa Uchina na ukimya wa Waislamu katika kuwatetea wenzao nchini humo.

Kampuni ya NetEase, ambayo inatoa video za PES nchini China, imesema kiungo huyo wa zamani wa timu ya taifa ya Ujerumani ameondolewa kwenye matoleo matatu yaliyopo nchini humo.

"Ozil ametoa matamshi makali kuhusu Uchina kwenye mitandao ya kijamii," imesema kampuni hiyo kwenye taarifa yake.

"Matamshi yake yameumiza hisia za mashabiki wa Kichina na kuvunja kanuni ya michezo ya amani na upendo. Hatuelewi, kukubali ama kusamehe jambo hili.

Arsenal imesema kuwa klabu hiyo "si ya kisiasa" na wizara ya mambo ya nje ya Uchina imedai kuwa mchezaji huyo mwenye asili ya Kituruki amedanganyika na habari za uongo za mtandaoni.

Makundi ya haki za binaamu yanadai kuwa takribani watu milioni moja - wengi wao kutoka jamii ya Waislamu ya Uighur - wanashikiliwa bila ya kufunguliwa mashtaka katika magereza yenye ulinzi mkali.

Uchina imekuwa ikikanusha kuwa inawanyanyasa Waislamu wa Uighur na kudai kuwa watu hao wanapatiwa mafunzo katika "vituo vya ufundi stadi" ili kukabiliana na ugaidi.

Kaibu Mkuu wa Baraza Kuu la Waislamu Uingereza, amesema Ozil ni wa "kupongezwa san" na kudai kuwa kitendo cha Arsenal kujitenga naye ni cha "kusikitisha".

-BBC