Amerika na Iran zapashana misuli

IRAN
IRAN
TAARIFA YA BBC

Marekani imeanzisha mashambulizi ya mtandao kwenye mifumo ya silaha za Iran siku ya Alhamisi wakati Rais wa Marekani Donald Trump alipoachana na mashambulizi ya anga, Ripoti nchini Marekani zimeeleza.

Mashambulizi hayo ya mtandaoni yameharibu mifumo ya kompyuta inayodhibiti roketi na mitambo ya kurushia makombora, limeeleza gazeti la Washington Post.

Tukio hilo ni kulipiza kisasi tukio la kushambuliwa kwa ndege yake isiyo na rubani pia mashambulizi dhidi ya meli za mafuta ambazo Iran imedaiwa na Marekani kuziteketeza,New York Times imeeleza.

Marekani pia imeweka vikwazo ambavyo rais Trump ameeleza kuwa ''vikubwa''.

Amesema vikwazo vilikua vinahitajika kuizuia Iran kutengeneza silaha za nyukilia na vikwazo vya kiuchumi vitaendelea mpaka pale Tehran itakapobadili uelekeo.

Mvutano kati ya Marekani na Iran ulijitokeza tangu Marekani ilipojiondoa kwenye mkataba wa nyukilia wa mwaka 2015 kati ya Iran na mataifa yenye nguvu duniani na kuiwekea vikwazo vilivyotikisa uchumi wa Iran.

Juma lililopita, Iran ilisema itaongeza viwango vilivyowekwa kwenye mkataba ule kuhusu mradi wa nyukilia.

Trump alisema hataki vita na Iran, lakini alionya kuwa Iran itakabiliwa na ''uharibifu'' ikiwa mzozo utatokea.

Mashambulizi yalipangwa kwa majuma kadhaa, vyanzo vimeviambia vyombo vya habari nchini Marekani ikaelezwa kuwa ni njia ya kulipa kisasi mashambulizi ya mabomu dhidi ya meli za mafuta kwenye Ghuba ya Oman.

Mashambulizi haya yamelenga mifumo ya silaha zinazotumiwa na majeshi ya nchi hiyo, yaliyoshambulia ndege isiyo na rubani ya rubani siku ya Alhamisi juma lililopita.

Kwa pamoja Washington Post na AP zimeeleza kuwa mashambulizi ya mtandao yameharibu mifumo.New York Times limesema ililenga kuzima mifumo hiyo kwa muda.

Siku ya Jumamosi duru za kiusalama za Marekani zilionya kuwa Iran ina mpango wa kufanya mashambulizi ya mtandaoni pia dhidi ya Marekani.

Chrostopher Krebs, Mkurugenzi shirika la usalama na miundombinu ya kiusalama nchini Marekani amesema ''hila za mashambulizi'' zinaelekezwa na utawala wa Iran na mawakala wake dhidi ya viwanda vya Marekani na mashirika ya kiserikali.

Iran pia imekuwa ikijaribu kudukua mifumo ya meli za kijeshi za Marekani, Washington Post limeripoti.

Hajasema chochote kuhusu ripoti za mashambulizi ya mitandaoni.Siku ya Ijumaa alisema ameacha mashambulizi ya anga dhidi ya Iran kwa sababu aliambiwa kuwa raia 150 watapoteza maisha.

Siku ya Jumamosi alisema alikua na mazungumzo ya wazi na raia wa Iran.

''kama Iran inataka kuwa taifa linalostawi...ni sawa kwangu, ''Trump alisema. ''Lakini hawatafikia hilo kama wanafikiri kuwa katika kipindi cha miaka mitano au sita watakuwa na silaha za nyukilia.

''Tuifanye Iran kuwa nzuri tena,'' aliongeza, akirejea kampeni yake ya mwaka 2016 wakati wa uchaguzi wa urais.