Ufaransa ilikuwa imefunga shule zote na taasisi za elimu ya juu tangia machi tarehe 17 kama njia ya kuzuia maambukizi zaidi ya virusi vya corona. Nchi hiyo imesajili visa zaidi ya 180,000 vya maambukizi ya corona huku watu zaidi ya elfu 28 wakiaga dunia kwa ajili ya ugonjwa huo kufikia Mei tarehe 18. Baada ya miezi miwili ya agizo la kutotoka nje nchi hiyo ilikuwa imeanza kuondoa masharti makali ili kuruhusu hali ya kawaida kurejelewa ikiwemo kufunguliwa kwa duka na shule za chekechea.
Licha ya kuwekwa mikakati ya kuwaruhusu wanafunzi kati ya 10 na 15 darasani, baadhi yao wameambukizwa virusi hivyo. Waziri wa elimu Jean-Michel Blanquer amekiambia kituo cha redio cha RTL kwamba visa 70 viilisajiliwa siku ya Jumatatu katika wiki ambayo shule zilifunguliwa akiongeza ni jambo ambalo halingeepukwa. Blanquer alisema visa 70 ni vichache sana kati ya wanafunzi milioni 1.4 waliorudi shule na kwamba shule zilizoathiriwa zitafungwa mara moja.
Ufaransa ni miongoni mwa mataifa kadhaa ya ulaya zikiwemo Ujerumani, Denmark, Norway, Poland na Jamhuri ya Czech ambazo zimelegeza masharti ya kuruhusu hali ya kawaida kurejea baada ya maagizo ya kutotoka nje na kuwabana watu kuendelea na shughuli za kawaida kwa takriban miezi mitatu.