•Victor amesema anajihisi tayari kuwakilisha wakazi wa Garissa huku akieleza imani yake kutwaa kiti hicho ambacho kwa sasa kinakaliwa na Abdulkadir Haji.
Mchekeshaji Victor Naman Omutula, anayejulikana sana kutokana na video zake za vichekesho za 'Ujinga za Victor Naman' ameonyesha nia yake ya kuingia seneti mwaka huu.
Mzaliwa huyo wa kaunti ya Kakamega ametumia kurasa zake za mitandao ya kijamii kutangaza azma yake ya kuwania kiti cha useneti cha Garissa.
Katika tangazo lake, Victor amesema anajihisi tayari kuwakilisha wakazi wa Garissa huku akieleza imani yake kutwaa kiti hicho ambacho kwa sasa kinakaliwa na Abdulkadir Haji.
"Sasa niko tayari kutumikia watu wa Garissa kwa cheo cha useneta. Hatuendei kingine ila ushindi tu. Anga ndio kikomo!" Victor amesema na kuambatanisha tangazo lake na bango la azma yake ya kuwa seneta.
Iwapo mchekeshaji huyo hafanyi mzaha juu ya suala hili, basi anajiunga na orodha kubwa inayoendelea kukua ya wasanii wanaomezea mate viti vya kisiasa.
MC Jessy, Jalang'o, Willy Paul, Prezzo na Rufftone ni baadhi ya wasanii wengine ambao wametangaza kujitosa kwenye siasa za 2022.