"Nampeza sana dadangu" Anerlisa Muigai amkumbuka dadake Tecra huku familia ikiadhimisha kifo chake

Muhtasari

•Bi Tecra aliaga mnamo Mei 2, 2020  kutokana na majeraha aliyoyapata baada ya kuanguka kutoka kwenye balcony ya nyumba ya familia huko Lamu.

•Anerlisa alionekana akiwa amebeba shada la maua na kuliwekelea juu ya kaburi la dadake kisha kusema maneno yasiyosikika.

Image: INSTAGRAM// ANERLISA MUIGAI

Familia ya mridhi wa Keroche Tecra Muigai iliadhimisha miaka miwili tangu kifo chake kilichotokea katika hali tatanishi. 

Bi Tecra aliaga mnamo Mei 2, 2020  kutokana na majeraha aliyoyapata baada ya kuanguka kutoka kwenye balcony ya nyumba ya familia huko Lamu.

Anerlisa Muigai alipakia picha kadhaa  za kumbukumbu zake na dadake na kuziambatanisha na jumbe maalum.

"Nampeza sana dadangu. Hii ni picha ya kwisho ambayo alipiga," Anerlisa aliandika chini ya picha yake akiwa amesimama kando ya picha ya dadake.

Mfanyibiashara huyo pia alipakia picha zake na wanafamilia wakitembelea kaburi la  marehemu wakati wa hafla ya kuadhimisha kifo chake.

Katika video moja, Anerlisa alionekana akiwa amebeba shada la maua na kuliwekelea juu ya kaburi la dadake. Baada ya kuweka maua yale Anerlisa alisema maneno yasiyosikika kwa kaburi hilo kisha kupiga sala.

"Natuma upendo kwa kila mtu ambaye amepoteza mpendwa. Sote tuko pamoja katika hili," Anerlisa aliandika chini ya video hiyo.

Marehemu Tecra alikuwa mtoto wa nne na wa mwisho wa mmiliki wa Keroche Breweries Tabitha Karanja.

Anerlisa alikuwa na uhusiano wa karibu mno na marehemu dadake mara nyingi amekuwa akionyesha wazi kuwa kifo hicho kilikuwa pigo kubwa kwake na bado hajaweza kukabiliana na hali ile.

Kitendawili kuhusu kifo cha Tecra bado hakijatatuliwa na miaka miwili baadaye bado kuna kesi inayoendelea mahakamani.