"Kuona mwili wako iliniumiza sana" Awinja amuomboleza muigizaji Maina Olwenya kwa ujumbe wa kihisia

Jacky alimtaja marehemu Olwenya kama msanii aliyekuwa na talanta kubwa

Muhtasari

•Jacky amekiri kuwa aliuumiza sana moyo wake kuona mwili wa muigizaji huyo mwenzake usio na uhai.

•Alimtaja marehemu Olwenya kama msanii aliyekuwa na talanta kubwa na kumtakia mapumziko ya amani.

Marehemu Maina Olwenya katika kikao cha awali na Jacky Vike
Image: INSTAGRAM// JACKY VIKE

Muigizaji Jacky Vike almaarufu Awinja kutokana na kipindi cha Papa Shirandula amemuomboleza marehemu Maina Olwenya.

Olwenya ambaye aliigiza katika filamu maarufu ya 'Nairobi Half Life' alizirai na kufariki dunia Jumatatu jioni.

Jacky amekiri kuwa aliuumiza sana moyo wake kuona mwili wa muigizaji huyo mwenzake usio na uhai.

"Mbaba!! Mbaba!! Aki mbaba ile kitu umetufanyia! 💔 Maneno yananishinda, kuona mwili wako usio na uhai jana iliniumiza sana!" Jacky alisema kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Mama huyo wa mtoto mmoja alimtaja marehemu Olwenya kama msanii aliyekuwa na talanta kubwa na kumtakia mapumziko ya amani.

"R.I.P tukutane kwenye hatua inayofuata Banyenjez, asante kwa kushiriki nasi talanta yako kali na isiyo na mfano! @mainaolwenya," Aliandika.

Wakati huohuo Jacky aliwasihi Wakenya kujitolea katika kuchanga pesa kwa ajili ya mazishi ya muigizaji huyo.

Mnamo Jumatatu Olwenya alianguka ndani ya nyumba yake na kukimbizwa hospitalini. Kufikishwa hospitali ilitangazwa kuwa amefariki.

Jumatano familia ya marehemu ilitoa taarifa kuhusu matokeo ya uchunguzi wa mwili kuhusu kilichosababisha kifo chake.

"Uchunguzi wa upasuaji wa maiti ulifanyika kwa mafanikio na matokeo yalikuwa kwamba marehemu Olwenya alikufa kutokana na Hypertrophic cardiomyopathy. Kwa maneno rahisi kulikuwa na kupungua kwa usambazaji wa damu kwa moyo kutokana na ugonjwa wa moyo ambao unaweza kusababisha na moyo kukosa kufanya kazi," Taarifa ilisoma.

Mipango ya mazishi ya msanii huyo ingali inaendelea huku matangazo ya tarehe rasmi na eneo la hafla hiyo yakisubiriwa.