“Pumzika kwa amani rafiki yangu” Gidi amuomboleza mwanamuziki mkongwe kwa hisia

Kunguru alifariki siku ya Jumapili baada ya kushambuliwa na ugonjwa.

Muhtasari

•Gidi amemuomboleza mwanamuziki mkongwe Eric Onguru almaarufu Kunguru ambaye aliaga dunia siku ya Jumapili.

•Kunguru aliaga dunia akiwa hospitalini ambako alikuwa amelazwa baada ya kushambuliwa na maradhi yasiyofichuliwa.

Mtangazaji Gidi amemuomboleza mwanamuziki Eric Onguru
Image: HISANI

Mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost Asubuhi kwenye Radio Jambo, Joseph Ogidi almaarufu Gidi amemuomboleza mwanamuziki mkongwe Eric Onguru almaarufu Kunguru ambaye aliaga dunia siku ya Jumapili.

Gidi ambaye waziwazi alionekana kushtushwa sana na kifo cha rapa huyo nguli alimuomboleza kama rafiki yake na kuitakia roho yake mapumziko ya amani.

"Eric Onguru almaarufu Kunguru ambaye aliimba 'Baby Don't Go' na Mr Lenny ameaga dunia. Pumzika kwa amani rafiki yangu," Gidi alisema kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii siku ya Jumapili.

Mtangazaji huyo mahiri ambaye pia alikuwa mwimbaji aliendelea kuashiria machungu yake kwa kumpoteza mmoja wa wenzake wa zamani katika tasnia ya muziki.

Kwa mujibu wa meneja wake wa zamani, Kunguru  alifariki siku ya Jumapili mwendo wa saa nane mchana. Marehemu alikuwa amelazwa katika Hospitali ya Nairobi kwa wiki chache zilizopita.

Meneja huyo wa zamani alieleza kuwa rapa huyo mkongwe amekuwa akilazwa na kuruhusiwa kuenda nyumbani mara kwa mara tangu mwaka wa 2017. Alihusisha ugonjwa wa Kunguru wa muda mrefu na ajali ya barabarabi aliyoipata mwaka wa 2009/10 ambayo iliathiri uti wake wa mgongo.

Kunguru anakumbukwa zaidi kwa nyimbo zake za  maarufu  "I Will Never Let you Go" na "Baby Don't Go", akimshirikisha Mr. Lenny.

Alianza kuimba akiwa na umri mdogo, ingawa alijizolea umaarufu mwaka wa 2006 ambapo aliachia African Woman akimshirikisha Mr Lenny.

Alikuwa mwanafamilia na pia alifanya kazi katika tasnia ya benki mbali na kazi yake ya muziki. Roho ya Kunguru ipumzike pema peponi.