Hisia zatawala huku Zari akimtambulisha mumewe Shakib kwa marehemu mama yake

Mamake Zari alifariki mwaka wa 2017, wiki kadhaa tu baada ya aliyekuwa mumewe, Ivan Semwanga kuzikwa.

Muhtasari

•Zari alionyesha video ya ziara ya kaburi la marehemu Halima Hassan ambapo aliandamana na Shakib, baba yake Nasur Hassan na mwanafamilia mwingine.

•Baadaye siku hiyo, wanandoa hao walitoka kwenda kwenye eneo la burudani nchini Uganda ambapo waliburudika pamoja.

Zari na mumewe Shakib katika eneo la burudani
Image: INSTAGRAM// ZARI HASSAN

Mwanasosholaiti maarufu wa Uganda Zari Hassan amemtambulisha rasmi mume wake Shakib Cham Lutaaya kwa marehemu mama yake.

Siku ya Alhamisi, mama huyo wa watoto watano  alichapisha video kadhaa za ziara ya kaburi la marehemu Halima Hassan ambapo aliandamana na Shakib, baba yake Nasur Hassan na mwanafamilia mwingine.

"Kumtambulisha mume wangu kwa marehemu mama yangu," alisema chini ya video moja ambayo alichapisha Instagram.

Katika video hiyo, yeye na Shakib walionekana wakiwa wamekaa kwenye kaburi la marehemu mama yake. Baba yake ambaye pia alikuwepo alionekana akiwa ameshika jiwe la kaburi huku akiwaambia maneno yasiyosikika.

Katika video nyingine, mzazi mwenza huyo wa Diamond alionyesha mazingira yanayozunguka kaburi ambapo msikiti wa babu yake pia upo.

"Nilikuja kumtembelea mama yangu, kaburi la mama yangu. Msikiti wa babu yangu. Bila shaka nilimleta mume wangu, kwa hivyo kutana na familia," Zari alisema kwenye video hiyo huku akionyesha mazingira ya karibu.

Baadaye siku hiyo, wanandoa hao walitoka kwenda kwenye eneo la burudani nchini Uganda ambapo waliburudika pamoja.

"Date night ambapo nilikabidhiwa na sanaa nzuri. Shukran mpenzi, ni nzuri. Hakika nilipenda, surprise iliyoje," alisema.

Zari alimtambulisha mumewe kwa marehemu mama yake.
Image: INSTAGRAM// ZARI HASSAN

Mamake Zari, marehemu Halima Hassan alifariki mwaka wa 2017, wiki kadhaa tu baada ya aliyekuwa mume wake, Ivan Semwanga kuaga dunia.

Takriban miaka sita iliyopita, muda si mrefu baada ya kumzika Ivan, Zari alipata habari kuwa mamake amelazwa hospitalini kutokana na ugonjwa wa moyo. Madaktari walifanya chochote walichoweza na akaruhusiwa kwenda nyumbani.

Lakini baada ya muda, alirudi hospitalini kwa majaribio zaidi. Zari alikuwa Uganda kwa muda wote ili kuhakikisha kwamba mzazi huyo wake anapata huduma na uangalizi wa kutosha. Hata hivyo, baadaye ilibidi asafiri kurudi Afrika Kusini kwa vile alikuwa amewaacha watoto wake huko. Lakini haikuchukua muda mrefu baada ya kuwasili huko ilipotangazwa kuwa mamake alikuwa ameaga dunia.

Alitumia mitandao ya kijamii kutangaza kifo cha mama yake akiandika, "Ni kwa masikitiko makubwa mimi na familia yangu tunatangaza kifo cha mama yetu mpendwa aliyefariki asubuhi ya leo. Roho yake ipumzike kwa amani, Mwenyezi Mungu akusamehe madhambi yako na akupe Janna.Utapendwa milele Jua letu la Kale, sisi kama watoto wako tulipewa kilicho bora zaidi kutoka kwa Mungu kama mama yetu. Tunashukuru kwa yote uliyotufanyia. Tutakuthamini daima Mama. Lala vizuri"