"Sijawahi ona kitenge kama hiyo!" Gidi astaajabishwa na vazi la harusi la mwanawe Gideon Moi

Mtangazaji Gidi amebainisha kwamba hajawahi kuona kitenge kama alichovaa Kigen.

Muhtasari

•Kigen alifunga ndoa na mchumba wake Rebecca Chepchumba katika harusi ya kitamaduni iliyofanyika  Kericho Jumamosi.

•Wanandoa hao na wapambe wa harusi walivalia mavazi ya kahawia yenye mabaka ya rangi ya chungwa.

wakati wa harusi yao siku ya Jumamosi.
Kigen Moi na mchumba wake Rebecca Chepchumba wakati wa harusi yao siku ya Jumamosi.
Image: HISANI

Mtangazaji wa kipindi cha Gidi na Ghost Asubuhi kwenye Radio Jambo, Gidi Ogidi amemwagia sifa kemkem mavazi yaliyovaliwa na mwanawe Gideon Moi, Kigen Moi wakati wa harusi yake mnamo siku ya Jumamosi.

Kigen alifunga ndoa na mchumba wake Rebecca Chepchumba katika harusi ya kitamaduni iliyofanyika katika kaunti ya  Kericho  siku ya  Jumamosi, Mei 6. Wageni kadhaa wakiwemo wanafamilia, marafiki wa karibu, wanasiasa na watu wengine mashuhuri walihudhuria hafla hiyo ya faragha.

Huku akizungumzia harusi hiyo ya kufana, mtangazaji Gidi alibainisha kwamba hajawahi kuona kitenge kama alichovaa Kigen.

"Hiyo arusi ya kijana ya Gideon, hiyo kitenge ni ya group of schools. Sijawahi ona kitenge kama hiyo. ama ni pesa inatoa kitenge hivo weuh 😂," Mtangazaji huyo wa kipindi cha asubuhi alisema siku ya Jumamosi.

Hii ilikuwa saa chache baada ya Kigen na Chepchumba kufunga pingu za maisha katika harusi nzuri ya kitamaduni. Wanandoa hao na wapambe wa harusi walivalia mavazi ya kahawia yenye mabaka ya rangi ya chungwa.

Jumamosi jioni, Gideon Moi alizamia kwenye Twitter kumpongeza Kigen na kumtakia yeye na mkewe mwongozo na baraka za Mungu.

"Ninajivunia mwanangu Kigen Moi kwa kupiga hatua kubwa katika maisha kwa kutafuta mkono wa Rebecca Chepchumba katika ndoa. Hakika, uchumba huu ni mradi mzuri wa kijamii na kiroho uliowekwa na Mungu kuhakikisha uchumba na mwendelezo," Kiongozi huyo wa chama cha KANU alisema.

Aliiongeza, ""Wanapoanza kurasimisha muungano wao leo (Jumamosi) katika Kaunti ya Kericho, ninaomba kwamba neema, mwongozo na baraka za Mungu ziwe juu yao kila wakati."

Aliyekuwa Waziri wa Nishati Charles Keter na aliyekuwa bosi wa NMS, Luteni Jenerali Mohamed Badi walihudhuria hafla hiyo.

Kigen ni mkurugenzi wa Sosian Energy Power Limited. Mwaka wa  2022, alitoa pikipiki kwa vyama vya boda boda katika maeneo mbalimbali ya Kaunti ya Baringo, kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa nafasi za kazi.