Mke wa Christian Atsu ashambuliwa kuhusu video ya densi baada ya kifo cha mumewe

"Siwezi kujipoteza, kwa sababu ninahitaji kuwa na nguvu kwa ajili ya watoto," Claire alisema.

Muhtasari

•Wakosoaji walimshambulia mkewe Atsu wakisema hakumpenda mumewe vya kutosha na kwamba hana huzuni kwamba alifariki.

•Mkewe Atsu alisema anapenda kucheza dansi na hiyo ni njia mojawapo ya yeye kukabiliana na huzuni yake.

akiwa na mke wake na watoto.
Mwanasoka marehemu Christian Atsu akiwa na mke wake na watoto.
Image: HISANI

Marie-Claire Rupio, mke wa marehemu mwanasoka Christian Atsu amewajibu wakosoaji waliomshambulia kwa kucheza densi.

Wakosoaji walijitokeza kwenye mitandao ya kijamii kumshambulia mama huyo wa watoto watatu wakisema hakumpenda mumewe vya kutosha na kwamba hana huzuni kwamba alifariki.

Claire alizungumza kupitia mitandao ya kijamii akisema anapenda kucheza dansi na hiyo ni njia mojawapo ya yeye kukabiliana na huzuni yake.

“Ni vizuri. Naandika ili niseme machache tu, ndiyo niliweka video ya ngoma, sio kwa sababu nimefurahi bali ni lazima nitafute namna ya kukabiliana na huzuni yangu, siko peke yangu, nina watoto 3 wa kutunza mwenyewe.

Siwezi kujipoteza, kwa sababu ninahitaji kuwa na nguvu kwa ajili yao.

Na huku Ulaya, unashughulikia afya ya akili kwa njia nyingi na dansi ilikuwa shauku yangu kila wakati.

Kwa hivyo samahani, lakini tafadhali fikiria kabla ya kuandika kitu au kuiweka kwenye YouTube," Marie-Claire alisema.

Aliongeza;

"Asanteni, Tunamkosa Christian kila siku na imekuwa si rahisi.

Hasa wakati una watoto 3, ambao kila siku wanamuuliza baba yao!

Ninajaribu kadri niwezavyo."

Christian Atsu,   alifariki mwezi Februari 2023 baada ya kuporomekewa na nyumba kufuatia tetemeko la ardhi lilipoikumba Uturuki.

Mzaliwa huyo wa Ghana alipatikana amefariki nyumbani kwake kusini mwa Uturuki. Alikuwa akiichezea klabu ya Hatayspor.

Winga huyo aliichezea timu ya taifa ya Ghana mara 65 na kuisaidia timu yake kufika fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika 2015.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 31 pia alichezea timu za Premier League Everton na Newcastle.

Alizikwa nchini Ghana.