Familia ya wapenzi mashuhuri nchini DJ Mo na mkewe msanii wa injili na mchunaji Size 8 leo Septemba 25 wamesherehekea miaka 10 tangu wafunge pingu za maisha.
Wawili hao walishiriki ujumbe wa pamoja kwenye mtandao wa Instagram na kusema kwamba haijakuwa safari rahisi ila kikubwa ni kwamba Mungu ndiye aliyechukua usukani kuwaongoza.
“Ni sherehe yetu ya MIAKA 10 YA NDOA leo.....😍❤️🎉 Tunamshukuru Mungu kwa matendo yake na tunatazamia miaka mingi zaidi katika ndoa kwa neema ya Mungu! UTUKUFU APEWE MUNGU......” Size 8 aliandika.
Msanii huyo ambaye miaka michache iliyopita alifuzu na kutawazwa kama mchungaji alisema kwamba bado hawajafika na huku mbele wanakoelekea bado watategemea mwongozo kutoka kwa Mungu na pia kuchukua fursa hiyo kuombea Baraka ndoa za mashabiki wake.
“Naomba Mungu awaaweke, awalinde, awape na kubariki ndoa zenu pia kwa jina la Yesu Kristo amina,” Size 8 alisema.
Wawili hao walifunga pingu za maisha mwaka 2013 na katika safari yao ya kifamilia licha ya umaarufu na kuonekana mitandaoni kwamba wako sawa, wamepitia changamoto si haba.
Katika mahojiano na Oga Obinna wiki chache zilizopita, DJ Mo alifichua kwamba wamewahi poteza ujauzito mara mbili.
Pamoja wana watoto wawili, msichana akiwa kifungua mimba na mvulana akiwa mdogo kwa sasa.
Mwaka jana kulivuja habari kwamba walikuwa wamekosana na kutengana kiasi kwamba Size 8 aliamua kuhama katika makazi yao na kwenda kuishi kando peke yake, jambo ambalo DJ Mo katika mahojiano hayo alikiri kwamba ni kweli lakini kikubwa wao hata wakosane vipi hurudisha hasira na majigambo chini na kuyasuluhisha.
Hii ndio ilikuwa familia ya pili kwa maceleb wa Kenya kuoana, baada ya watu kuzoea kwa takribani miaka 9 familia ya Nameless na mke wake Wahu ambao pia wiki chache zilizopita walitimiza miaka 18 katika ndoa.
Nameless na Wahu walifunga ndoa yao mwaka 2005.