Sandra Dacha atoa taarifa ya kutia wasiwasi kuhusu afya ya Akuku Danger

Muhtasari

•Dacha amemlilia Maulana kuingilia kati na kumponya mwandani  huyo wake huku akisema Akuku  Danger hastahili kupatwa na shida zote za kiafya zinazomkabili kwa sasa.

Sandra Dacha atoa taarifa ya kutia wasiwasi kuhusu afya ya Akuku Danger
Sandra Dacha atoa taarifa ya kutia wasiwasi kuhusu afya ya Akuku Danger
Image: INSTAGRAM

Inaonekana mchekeshaji wa Churchill Show Akuku Danger hakuruhusiwa kutoka hospitalini siku ya Jumamosi kama ilivyotabiriwa hapo awali na rafiki yake wa karibu Sandra Dacha almaarufu kama Silprosa.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Dacha sasa ameripoti kwamba mchekeshaji huyo amegundulika kuwa na tatizo la moyo.

Mwigizaji huyo wa kipindi cha Auntie Boss amemlilia Maulana kuingilia kati na kumponya mwandani  huyo wake huku akisema Akuku  Danger hastahili kupatwa na shida zote za kiafya zinazomkabili kwa sasa.

"Maambukizi ya moyo sasa tena imetoka wapi saa hii jameni. Mungu mpendwa, anahitaji kurudi nyumbani kwake. Tafadhali mponye. Mungu mpendwa , Akuku Danger hastahili magonjwa haya yote.. ni mengi sana kwake. Muonee huruma na umponye arudi kwa nyumba yake" Dacha ameandika.

Siku chache zilizopita Dacha alitangaza kwamba Akuku Danger angeruhusiwa kutoka hospitali mnamo Jumamosi.(Januari 15, 2021)

Alitoa wito kwa Wakenya kuendelea kuchangia bili ya hospitali ya mchekeshaji huyo ili kumwezesha kuachiliwa  kwenda nyumbani.

"Tafadhali tusaidieni kupeleka Akuku Danger nyumbani, tafadhali. Ataruhusiwa kwenda nyumbani kesho. Paybill 891300 ACC (Weka jina lako)" Dacha alisema.

Dacha amesihi Wakenya kuendelea kumchangia rafikiye kwani bili ya hospitali inaendelea kupanda kila uchao.