Diamond Platnumz afichua gharama kubwa ya mapambo yake ya mkono

Muhtasari

•Ameonyesha mapambo maridadi ya mikono yake na kueleza kwamba yalimgharimu dola laki mbili ambazo  ni sawa na shilingi milioni 23 za Kenya.

•Mapambo hayo ni pamoja na saa, bangili tano na pete kumi zote ambazo zilionekana kutengenezwa na vito vyenye thamani kubwa.

Image: INSTAGRAM// DIAMOND PLATNUMZ

Utajiri mkubwa wa mwanamuziki Naseeb Abdul Juma almaarufu kama Diamond Platnumz sio jambo la kutilia shaka. 

Nyota huyo wa Bongo anaaminika kuwa miongoni mwa wasanii tajiri zaidi, sio tu nchini Tanzania alikotoka bali pia barani Afrika na hata kote ulimwenguni.

Diamond anajulikana kutoficha utajiri wake na mara kadhaa ameonekana akianika mali yake ya thamani kwenye mitandao ya kijamii.

Kwenye ukurasa wake wa Instagram, baba huyo wa watoto wanne wanaojulikana ameonyesha mapambo maridadi ya mikono yake na kueleza kwamba yalimgharimu dola laki mbili ambazo  ni sawa na shilingi milioni 23 za Kenya.

Mapambo hayo ni pamoja na saa, bangili tano na pete kumi zote ambazo zilionekana kutengenezwa na vito vyenye thamani kubwa.

"Dola 200,000 kwa vidole. Simba, Chibu" Diamond aliandika kwenye video ambayo alichapisha.

Haya yanajiri wiki chache tu baada ya msanii huyo mwenye umaarufu mkubwa kote Afrika kumnunulia mamake, Mama Dangote mkufu wenye thamani ya shilingi milioni 5.4 za Kenya.

Mama Dangote alielezea furaha yake  kubwa baada ya mwanawe kumnunulia mkufu huo maridadi kama zawadi huku akisema anajivunia kumzaa Diamond.

"Kuzaa kuzuri asante baba yangu Naseeb, nakupenda sana." Mama Dangote alisema

Takriban miezi miwili iliyopita Mama Dangote pamoja na mpenzi wake Uncle Shamte walifichua kwamba kufikia sasa Diamond anamiliki nyumba na viwanja zaidi ya 67 nchini Tanzania.