"Ni mke wangu yule!" Alikiba awafokea wanaouliza kuhusu talaka

Muhtasari

• Naona mna haja sana ya kusikia mambo ya watu na ndoa zao. Hayawahusu. Ni mke wangu yule, wee mke wako? Umesikia nikikuuliza swali la mke wako? - Alikiba alifoka

Alikiba akimvisha pete mkewe Amina Khalef
Alikiba akimvisha pete mkewe Amina Khalef
Image: THE STAR

Ni habari mpya kwa mashabiki wa msanii Alikiba baada ya msanii huyo kudokeza kwamba huenda walisuluhisha tofauti zilizokuwepo zinayumbisha ndoa yake na mkewe na sasa pengine hali ya mawimbi kidogo imetulia.

Hii ni baada ya msanii huyo kuwafokea kwa ghadhabu wanablogu waliojaribu kumuuliza kuhusu ishu hiyo ya kutalikiana na kuwaambia kwamba huyo bado ni mke wake na katu hatoruhusu kauli za kuwakosanisha kutoka kwa watu wa hovyo mitandaoni.

Alikiba alikuwa akiyazungumza hayo katika uzinduzi wa albamu ya msanii mwenza Rich Mavoko ambapo katika mkutano na wanahabari aliulizwa baadhi ya maswali na lilipofika hilo la familia yake, Alikiba akipandwa na mori kweli mpaka kutaka kutupa masumbwi.

“Ali, hivi karibuni kulitokea vurugu kati yako wewe na mkeo, na ilisemekana kwamba mke wako alienda mahakamani kudai talaka. Na kuna story kwamba kwa sasa mmesameheana na mkeo, hebu tuambie ni ukweli ama ni porojo,” mwanahabari mmoja alimuuliza.

“Naona mna haja sana ya kusikia mambo ya watu na ndoa zao. Hayawahusu. Ni mke wangu yule, wee mke wako? Umesikia nikikuuliza swali la mke wako?” Alikiba alipandwa na ghadhabu huku akiondoka kwenye kikao hicho.

Mwezi miwili iliyopita palisambaa uvumi kwamba Amina Khalef alikuwa ameachana na staa huyo wa bongo fleva na kurudi kwao Kenya ambapo inasemekana alielekea katika mahakama ya Kadhi kutaka talaka kutoka kwa msanii huyo.

Uvumi huo ulipatiwa uhai hata zaidi baada ya Kiba kumtakia kheri njema ya siku ya kuzaliwa mwanawe kwa ujumbe wenye ukakasi ambapo alimtaka asimsahau, jambo lililopelekea majasusi wa mitandaoni kusema kwamba hawako tena pamoja na hangekuwa na uwezo wa kuona wanawe kwa sababu ya kutalikiana na mama watoto.