Kutana na mapacha watatu wanaochumbiana na jamaa mmoja

Muhtasari

•Mapacha hao walisema walipokutana na jamaa huyo waliungana vizuri naye na akakubali kuwachumbia wote watatu.

•Waliweka wazi kuwa hakuna uwezekano wa yeyote kati yao kumwonea gere mwenzake kwa kuwa wamekuwa na uhusiano mzuri tangu kuzaliwa kwao.

Image: INSTAGRAM// COMRADES TRIPLETS

Dada watatu wamekuwa gumzo kwenye mtandao baada yao kujitokeza na kufichua kuwa wote wanamchumbia jamaa mmoja.

Catherine, Mary na Eve ambao ni mapacha wanaofanana kama shilingi kwa ya pili wamekiri kuwa walivutiwa sana na mwanavlogu mmoja wa hapa nchini na wakapiga hatua ya kujuana naye zaidi.

"Nilikuwa namtazama kwenye YouTube. Siku moja nikaonyesha Mary nakamwambia huyo jamaa huwa ameweza. Vile nilimwambia akasema kweli ako poa. Hatukuwa tunajua kuhusu Eve, kumbe aliweka siri tu. Vile tulizua suala hiyo akasema huyo jamaa ako poa," Catherine alieleza wakiwa kwenye mahojiano na Jalang'o.

Mapacha hao walisema walipokutana na jamaa huyo waliungana vizuri naye na akakubali kuwachumbia wote watatu.

Walisema tayari wamekubali kufunga pingu za maisha na jamaa huyo wote pamoja na kufichua kwamba mipango ya jinsi ndoa yao itakuwa bado inaendelea.

"Bado tunapanga. Jumatatu atakuwa na mmoja wetu, Jumanne anachukua mwingine, Jumatano anachukua huyo mwingine," Walisema.

Waliweka wazi kuwa hakuna uwezekano wa yeyote kati yao kumwonea gere mwenzake kwa kuwa wamekuwa na uhusiano mzuri tangu kuzaliwa kwao.

"Tulimwambia atupende sawa. Bora asipende mmoja kuliko mwingine. Tayari amejua kututambua lakini wakati mwingine tunaweza kumchanganya," Mapacha hao walieleza.

Mapacha hao walisema jamaa anayeachumbia amekubali kulipa mahari yao wote na kudai kwamba tayari ameanza kujipanga.

Walisema wamekuwa pamoja kwa maisha yao yote na hata walihudhuria shule moja ya msingi na ya upili. Walifichua kuwa hisia zao wote huwiana zikiwemo hisia za kimapenzi.