Amira hatimaye ajibu baada ya mumewe Jimal Rohosafi kujuta kumkosea na kuomba msamaha

"Wacha nirudi ndo ni address the nation nikiwa homeground!" Amira amesema.

Muhtasari

•Jimal aliandika ujumbe mrefu wa kuomba msamaha kwa mkewe na kukiri kuwa alimkosea sana kwa kuingiza drama nyingi kwenye ndoa yao ya miaka mingi.

•Amira ambaye amekuwa Tanzania amesema  atahutubia watu kuhusiana na suala hilo pindi atakaporejea nchini.

Image: INSTAGRAM// BEING AMIRA, JIMAL MARLOW ROHOSAFI

Hatimaye mfanyibiashara Amira ametoa jibu la kwanza baada ya mumewe Jimal Marlow Rohosafi  kumuomba msamaha hadharani.

Jumamosi Jimal aliandika ujumbe mrefu wa kuomba msamaha kwa mkewe na kukiri kuwa alimkosea sana mama huyo wa watoto wake wawili kwa kuingiza drama nyingi kwenye ndoa yao ya miaka mingi.

"Naomba radhi kwa kukukosea heshima, kukuaibisha, kwa kukuumiza, kwa maumivu yote na kwa huzuni niliyokuletea. 💔Samahani kwa nyakati zote ambazo sijawa mwanaume niliyeahidi kuwa," Jamal alimuandikia mkewe.

Mwenyekiti huyo wa Muungano wa Wamiliki Matatu jijini Nairob alikiri kwamba alikosa kutimiza  wajibu wake wa kumlinda mkewe kama alivyohitajika kufanya.

Aidha alikiri kuwa  alifahamu wakati ndoa yake ikiporomoka ila akashindwa na la kufanya kwa wakati ule.

"Ilikuwa mbaya kabisa. Huenda nilionekana kama mtu asiye na wasiwasi lakini sikuwa na la kufanya. Nilijua haikuwa sawa, nilijua unaumia lakini sikuweza kujikusanya!Amira nafanya hivi kwa sababu ukosefu wa heshima pia ulikuwa mkubwa. Naomba radhi kwa kukosa heshima," Aliandika.

Jimal pia alifichua kuwa hajakuwa sawa tangu alipokosana na mke huyo wake. Pia alidokeza kuwa yupo tayari kupiga hatua zozote ili kufufua ndoa yao iliyokufa miezi kadhaa iliyopita.

"Tafadhali nisamehe. Mimi na wewe tumetoka mbali na kukupitishia kwa yote hayo hakukuwa kuzuri. Tafadhali nisamehe Amira,"

Sasa ni wazi kuwa ujumbe huo ulimfikia mlengwa kwani siku moja baadae amechapisha ujumbe unaodokeza kuwa yupo tayari kutoa jibu lake.

Mama huyo wa watoto wawili ambaye katika kipindi cha siku kadhaa ambacho kimepita amekuwa nchini Tanzania ameeleza kuwa atahutubia watu kuhusiana na suala hilo pindi atakaporejea nchini.

"Wacha nirudi ndo ni address the nation nikiwa homeground!" Amira aliandika kwenye Instastori zake.

Isitoshe, alifuatisha na video zilizoonyesha akiwa katika uwanja wa ndege, ishara kuwa tayari yupo njiani kurudi nyumbani.

Kwa kweli wambea wamesubiri kwa hamu na gamu kuona ikiwa mfanyibiashara huyo atakubali kumsamehe mumewe.

Mwezi Novemba mwaka uliopita Amira alianza mikakati ya kutafuta talaka baada ya mumewe kumtema na kugura na mwanasoshalaiti Amber Ray.