Diamond afichua asili ya jina lake la utani 'Chibu Dangote'

Diamond alikiri kuwa 'Dangote' ni jina la majigambo kufuatia utajiri wake mkubwa

Muhtasari

•Diamond ambaye jina lake halisi ni Naseeb Abdul Juma ana majina mengi ya utani yakiwemo Chibu Dangote, Simba, Lion of Africa na Mondi.

•Alifichua kuwa aliongeza jina la Dangote kwa Chibu kama njia ya kujigamba kuhusu utajiri wake mkubwa.

wakiwa ziarani
Diamond Platnumz na meneja wake Sallam SK wakiwa ziarani
Image: INSTAGRAM// DIAMOND PLATNUMZ

Staa wa muziki Bongo, Diamond Platnumz amefunguka kuhusu asili ya jina lake moja la utani ‘Chibu Dangote’.

Diamond ambaye jina lake halisi ni Naseeb Abdul Juma ana majina mengi ya utani yakiwemo Chibu Dangote, Simba, Lion of Africa, Mondi na mengineo.

Akiwa kwenye mahojiano na DW Afrika, Mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 32 alifichua kuwa 'Chibu' ni jina lake la utani kutoka utotoni.

Bosi huyo wa WCB alieleza kuwa alipokuwa mtoto hakuweza kulitamka vizuri jina lake 'Naseeb'  na badala yake alilitamka kama 'Chibu', hivyo likawa jina lake la utani.

"Chibu ni Naseeb. Jina langu halisi ni Naseeb. Nikiwa mtoto mdogo singeweza kutamka jina Naseeb. Nilikuwa najiita Chibu. Nikiulizwa jina langu nilikuwa nasema Chibu," Diamond alisema.

Aidha alifichua kuwa aliongeza jina la Dangote kwa Chibu kama njia ya kujigamba kuhusu utajiri wake mkubwa.

"Dangote ni kama jina la kujigamba. Mfano, wengine wanajiita Mendez Don. Badala ya kujiita Don nikajiita Dangote. Dangote inaamanisha nawakilisha Afrika. Lazima tujivunie watu tulio nao.Lazima tujivunie kitu kitu tulicho nacho. Badala ya kujiita  Chibu the Don nikajiita Chibu Dangote kushiria nawakilisha pesa," Alisema.

Katika mahojiano hayo Diamond alimbwagia sifa kochokocho mama yake, Mama Dangote. Alieleza kuwa mama yake, Mama Dangote ndiye aliyemuwezesha kufika alipo sasa.

"Nampenda mamangu na nataka tu kumfanya afurahi. Huwa najaribu kumweleza jinsi ninavyompenda na najivunia aliyonifanyia," Alisema wakati alipoulizwa sababu za kumtaja mamake kwenye nyimbo zake.

Katika siku za hivi majuzi staa huyo wa muziki amekuwa akifanya ziara za kikazi katika mataifa mbalimbali ya Ulaya.

Kwa sasa Diamond anaaminika kuwa miongoni mwa wasanii maarufu na tajiri zaidi barani Afrika akiwekwa kwenye orodha moja na wababe wengine kama Burna Boy na Davido kutoka Nigeria.