"Pongezi rais Ruto, uongozi Mungu amekupa!" - Justina Syokau amtungia Ruto wimbo

“Sio juju ni maombi, tumeona mkono wa bwana, pongezi rais Ruto" - Justina Wamae aliimba.

Muhtasari

• Msanii huyo alipata umaarufu alipotoa wimbo wa mwaka 2020 ulioshabikiwa na wengi kabla ya janga la Korona kubisha.

Mwanamuziki huyo ameachia kibao kipya cha kumpongeza rais Ruto
Justina Syokau na WilliamRuto Mwanamuziki huyo ameachia kibao kipya cha kumpongeza rais Ruto
Image: Maktaba, YouTube screengrab

Mwanamuziki mwenye utata Justina Syokau ametoa wimbo wa kumpongeza rais mteule William na kumsherehekea kwa ushindi.

Syokau ameachia kibao hicho yapata siku nne baada ya mahakama ya upeo kuidhinisha ushindi wa Ruto kama rais wa 5 kwa kutupilia mbali ombi la Azimio lililotaka ushindi huo kubatilishwa.

Katika wimbo huo ambao Justina Syokau ameupakia kwenye YouTube yake Alhamis adhuhuri, anasikika akitumia baadhi ya misemo ambayo wanasiasa kutoka mrengo wa Kenya Kwanza walikuwa wanatumia kujipigia debe kipindi cha kampeni.

Wimbo huo unaitwa Pongezi rais Ruto.

“Sio juju ni maombi, tumeona mkono wa bwana. Tumepata rais wa 5 hapa Kenya Mungu amejibu maombi. Pongezi rais wetu Ruto uongozi Mungu amekupatia. Ni Mungu amekumwagilia mafuta maana uongozi unatoka kwake,” baadhi ya mistari kwenye wimbo huo wa Justina Syokau inasema.

Syokau ambaye ana utata asijulikane anaimba nyimba zipi kati ya zile za kidunia au za injili si mara ya kwanza kuachia wimbo wenye maudhui maalumu.

Itakumbukwa aligongwa vichwa vya habari na hata kujulikana na wengi mpaka kuramba madili ya kuwa balozi wa mauzo katika kampuni mbali mbali mwaka 2020 alipoachia kibao cha mwaka 2020 kilichowafurahisha wengi sana kabla ya janga la Korona kuvuruga mwaka huo.

Mwanamuziki huyo pia alikuja akaachia kibao kingine cha kusherehekea miaka mingine iliyofuata.

William Ruto anatarajiwa kuapishwa kama rais wa tano wa Kenya mnamo Septemba 13 katika uwanja wa Moi Kasarani, jijini Nairobi na wengi wamesema Justina amefanya ndivyo kujitongozea nafasi japo kutumbuiza wageni waalikwa katika hafla hiyo ya kitaifa kupitia huu wimbo wake mpya.