• Wiki moja baada ya kushinda alipakia video akiomba watu asiowajua waache kumsumbua yeye na familia yake.
Mshindi wa bahati nasibu wa India anakiri sasa analemewa sana na maombi ya watu wakimwomba usaidizi wa kifedha ila sasa anajuta kupata jakipoti hiyo.
Anoop Babu ambaye ni dereva wa magari kutoka jimbo la Kerala, alishinda Rupi milioni 250 ambazo ni katika bahati nasibu ya serikali ya jimbo mapema Septemba mwaka huu.
Lakini wiki moja baadaye, alichapisha video akiomba watu asiowajua waache kumsumbua yeye na familia yake.
Hata hivyo, Anoop amedai inamlazimu kuhama nyumba kila mara ili kuepuka unyanyasaji kutoka kwa watu asiowajua wanaomsaka wakitaka msaada wa pesa.
Waandishi wa vyombo vya habari walijitokeza nyumbani kwake ili kumwaangazia na familia yake jambo ambalo halijamridhisha.
''Laiti nisingeshinda," anasema.
Anoop anasema kwenye video hiyo kwamba anafikiria kuhama anakoishi ili kuepuka kusemangwa na umma na kuangaziwa kila wakati na vyombo vya habari.
Jamaa huyu aligonga vichwa vya habari vya kitaifa aliposhinda tuzo ya juu zaidi kuwahi kutolewa jimboni katika mchezo wa bahati nasibu.
Alinunua tikiti mnamo tarehe 18 Septemba siku moja kabla ya kusafiri hadi Malaysia kwa minajili ya kazi baada ya kuchukuwa akiba ya mwanawe.
Baada ya habari kuibuka za ushindi wake, familia yake ililengwa sana na vyombo vya habari.
"Nilifurahi sana niliposhinda," anasema kwenye video hiyo iliyovuma Facebook. "Lakini sasa hali imekuwa ngumu sana", anasema.
"Siwezi kutoka nyumbani, siwezi kwenda popote. Mtoto wangu ni mgonjwa na siwezi kumpeleka kwa daktari." Anoop aliongeza
Serikali ya jimbo hilo sasa inampa mafunzo ya siku moja ili kumsaidia kutumia pesa hizo vizuri. Anoop alipokea rupi milioni 150 baada ya ushuru.
Amesema kuwa baada ya kushinda jakipoti hiyo, alipania kufungua mgahawa.