(+video) Mwanadada avunjwa moyo na kitendo cha mamake kumnyoa mtoto wake

Mwanadada huyo alielezea kumwaacha mtoto na mamake na aliporudi akapata nywele zote zimenyolewa kichwani mwa mtoto.

Muhtasari

• Nilichofanya ni kucheka tu kwa sababu yeye ni mama yangu, nywele zitakua tena - Alisema.

Kila mama hupenda kuona nywele ya mwanawe haswa akiwa mchanga ikiwa inapendeza, kutokana na dhana kuwa nywele za kuzaliwa aghalabu huwa nyepesi na laini kupendeza mno.

Mwanamke mmoja amepeleka kwenye Tiktok akiteta na kuonesha kuvunjika moyo na kitendo cha mamake kumnyoa mtoto wake nywele zote ambazo amekuwa nazo tangu kuzaliwa.

Katika video hiyo iliyojumuisha msururu wa picha za mwanawe wa kiume tangu akiwa mdogo mpaka wakati alinyolewa na nyanya yake akiwa na takribani miaka 3-4, mtoto huyo alionekana amenyolewa kabisa hadi huwezi ukatofautifa kichwa na uso vimetengania wapi.

Akieleza kuvunjika kwake moyo, mwanadada huyo alisema kwamba moyo wake mpaka sasa unauma akiona picha za zamani za kijana wake akiwa na nywele laini zilizokuwa zikimtiririka kutoka kichwani hadi mabegani kama manyoya ya farasi.

Alieleza kuwa kitendo cha mwanawe kunyolewa kilitokea wakati alimuacha na mama yake ambaye kwa mtoto huyo ni nyanya, aliporudi akapata kichwa kinamtabasamia kwa utupu wa nywele.

“Oi, moyo wangu bado unauma, mtoto wangu amekuwa na nywele fulani nzuri tu tangu kuzaliwa. Halafu siku moja nilimuacha na mamangu nikienda chuo. Kurudi nikapata amemnyoa nywele zote,” Mwanamke huyo alieleza kwa masikitiko makubwa.

Alisema kwamba hangeweza kumkasirikia mama yake kwa kitendo kile kwa sababu ni mjukuu wake alikuwa ananadhifisha ila ndani kwa ndani kitendo kile kilimuuma kweli.

“Nilichofanya ni kucheka tu kwa sababu yeye ni mama yangu, nywele zitakua tena 😭😭😭😭 nyie mnaowakandia wazazi, kesi ya kuzimu kuna joto acha mama zenu 🤣🤣” aliandika.