Mama Shahrukh! Mwimbaji Ray C abarikiwa na mtoto wa kwanza

"Naitwa Mama Shahrukh #AsanteMungu," alisema.

Muhtasari

•Mwimbaji huyo wa kibao 'Mama Nitilie' alifichua kwamba alijifungua mtoto wa kiume na kumpa jina Shahrukh.

•Mwanamuziki huyo alifichua ujauzito wake mnamo Februari 7, na kuelezea jinsi alivyojitahidi kuuweka siri.

Image: INSTAGRAM// RAY C

Mwimbaji wa Bongofleva Rehema  Chalamila almaarufu Ray C amemkaribisha duniani mtoto wake wa kwanza.

Wakati akitangaza habari hizo njema kwenye ukurasa wake wa Instagram siku ya Jumatatu, mwimbaji huyo wa kibao 'Mama Nitilie' alifichua kwamba alijifungua mtoto wa kiume na kumpa jina Shahrukh.

"Naitwa Mama Shahrukh #AsanteMungu," aliandika.

Aliambatanisha ujumbe huo mfupi na picha ya kitoto kichanga kikiwa kimelazwa kwenye kitanda. Uso wa mtoto huyo hata hivyo ulikuwa umefichwa.

Mwanamuziki huyo alifichua ujauzito wake mnamo Februari 7, na kuelezea jinsi alivyojitahidi kuuweka siri.

Kwenye ukurasa wake wa Instagram, Ray C alichapisha video iliyoonyesha tumbo lake likiwa limechomoza sana.

"Wakati wa Mungu ni wakati sahihi," aliandika chini ya video hiyo.

Mwimbaji huyo kwa sasa anaishi na mume wake mzungu nchini Ufaransa. Alihamia nchi hiyo ya Ulaya miaka michache iliyopita na kwa muda mrefu amekuwa akiweka maisha yake ya kibinafsi kuwa siri.

Shahrukh ni mtoto wa kwanza wa Ray C. Takriban miaka minne iliyopita alifunguka kuhusu ujauzito wake kuharibika.

"Naombeni ushauri kina mama wote nifanyaje mimba isitoke? imeniuma imenibidi nishee nanyi  #mtotowanguhayupo tena  #mwanangukaendazake," aliandika kwenye mitandao ya kijamii.

Kwa muda mrefu, mwimbaji huyo alipambana na uraibu wa dawa za kulevya ambao uliharibu kazi yake ya muziki iliyokuwa ikisitawi kwa karibu muongo mmoja.

Alipelekwa rehab na aliyekuwa Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete. Baadaye alijitahidi kurudi tena katika tasnia ya muziki lakini hakufanikiwa kupata utukufu wake uliopotea.