Mchekeshaji KK Mwenyewe alazwa hospitalini baada ya kujaribu kula kilo moja ya pilipili

“Nawekwa maji. Daktari alisema nilihara sana. Naskia tumbo ikiwa kali. Minyoo inaskia ni kama iko jehanamu,” alisema.

Muhtasari

•Mchekeshaji huyo alionekana akihangaika kumeza pilipili na hakuweza hata kumaliza vijiko viwili vya tunda hilo kali.

•Ameweka wazi hatawahi kujaribu kitu kama hicho tena na akatangaza kwamba hatashabikia tena mpira wa miguu.

Image: INSTAGRAM// KK MWENYEWE

Mchekeshaji maarufu wa Kenya Zachariah Kariuki almaarufu KK Mwenyewe anadaiwa kulazwa hospitalini siku ya Ijumaa baada ya kula pilipili nyingi.

Mchekeshaji huyo ambaye anajulikana zaidi kwa kumuiga naibu rais Rigathi Gachagua mnamo Alhamisi aliapa kula kilo nzima ya pilipili ikiwa timu yake anayoipenda zaidi, Manchester United ingeshindwa na Chelsea.

Huzuni kwake, Mashetani Wekundu walichapwa 4-3 katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja wa Stamford Bridge Alhamisi usiku na alilazimika kutimiza ahadi yake kwa mashabiki wake.

“Kama nilivyoahidi, nitakula kilo nzima ya pilipili. Sijui kitakachotokea lakini tuanze,” KK alisema kwenye picha ambayo alishiriki usiku wa kuamkia Ijumaa iliyomuonyesha akiwa ameshikilia sahani ya pilipili.

Pia alishare video iliyomuonyesha akila viungo hivyo  vikali na kuweka wazi kuwa hafahamu matokeo ya hatua yake hiyo.

Katika video hiyo, mchekeshaji huyo alionekana akihangaika kumeza pilipili na hakuweza hata kumaliza vijiko viwili vya tunda hilo kali.

Baada ya kushindwa kuendelea, alionekana akinywa soda pengine kuondoa ukali mdomoni mwake. Pia alionekana akijaribu kupiga mswaki, na kula sukari nyingi ili kuondoa ladha kali.

Baadaye siku ya Ijumaa, mchekeshaji huyo alishiriki video ikionyesha kana kwamba alikuwa amelazwa kwenye kitanda cha hospitali akipokea matibabu.

“Nawekwa maji. Daktari alisema nilihara sana. Naskia tumbo ikiwa kali. Minyoo inaskia ni kama iko jehanamu,” alisikika KK akimwambia rafiki yake.

“Presha ilikuwa juu na damu ilikuwa imeenda sana. Nimepoteza maji, wamesema nimepoteza kilo saba ya maji.. Madaktari wamesema sio mbaya. Lakini naskia sijui nilizie hizo pilipili ama... ” aliongeza.

Kufuatia matokeo hayo mabaya, mchekeshaji huyo aliweka wazi kuwa hatawahi kujaribu kitu kama hicho tena na pia akatangaza kwamba hatashabikia tena mpira wa miguu.