Amber Ray afunguka sababu zake kusonga mbele haraka baada ya kukosana na wapenzi wake

Muhtasari

•Amber Ray alifichua kwamba hakuna uhasama wowote kati yake na mpenzi wake wa hivi majuzi Jimal Rohosafi.

•Mwanasoshalaiti huyo alisema kwa kawaida huwa hapotezi wakati wake kulia juu ya mahusiano yake yaliyogonga ukuta.

Amber Ray na Jimal Rohosafi
Amber Ray na Jimal Rohosafi
Image: INSTAGRAM

Mwanasoshalaiti Faith Makau almaarufu kama Amber Ray ameweka wazi kwamba bado huwa anawasiliana na wapenzi wake wengi  wa zamani.

Akizungumza na waandishi wa habari katika hafla ya kuzindua lebo yake, Amber Ray alisema wapenzi wake wengi wa zamani ni marafiki wake wa karibu kwa sasa.

"Mwanzoni wao huwa na uchungu mwingi. Kadri siku zinavyosonga wao huzoea. Mimi ni mkweli sana. Nipo karibu sana na wengi wao. Wao ni miongoni mwa watu ambao naweza kupigia nikipata shida na wanisaidie wakati wowote," Amber Ray alisema.

Mama huyo wa mtoto mmoja alifichua kwamba hakuna uhasama wowote kati yake na mpenzi wake wa hivi majuzi Jimal Rohosafi.

Amber Ray hata hivyo aliweka wazi kwamba hajarudiana na mwenyekiti huyo wa wamiliki wa matatu jijini Nairobi.

"Huwa tunazungumza. Sisi sio maadui. Haikufanya kazi lakini sisi sio maadui," Alisema.

Mwanasoshalaiti huyo alisema kwa kawaida huwa hapotezi wakati wake kulia juu ya mahusiano yake yaliyogonga ukuta.

"Mbona nipoteze muda nikilia juu ya mtu. Sijui wanafanya nini na maisha yao. Kwangu mstari hauna mwisho," Alisema.

Alitangaza kwamba mahusiano yake na mchezaji mpira wa vikapu kutoka Sierra Leone, Ib Kabba yalifika hatima.Alisema kwa sasa hachumbiani na mwanaume yeyote.