Andrew Kibe na Jalang’o washiriki mazungumzo, wafunguka ukweli kuhusu ugomvi wao

Wawili hao walifichua kwamba hawakuwahi kuzozana hapo awali na hata waliwahi kulewa pamoja mara nyingi.

Muhtasari

•Mazungumzo yao yalipokuwa yakiendelea, Jalang'o alimuuliza mtumbuizaji huyo kwa nini anamchukia sana.

•Kibe aliweka wazi kuwa alisherehekea uvumi wa kushindwa kwa Jalang'o kwa sababu alikuwa amesema uwongo kumhusu.

Jalang'o na Andrew Kibe
Image: HISANI

Muundaji maudhui Andrew Kibe na mbunge wa Lang'ata Phelix 'Jalang'o' Odiwour wamebainisha kwamba kuna uhusiano mzuri kati yao.

Wawili hao ambao wameonekana kuzozana katika siku za nyuma walishiriki mazungumzo ya moja kwa moja mtandaoni siku ya  Alhamisi jioni ambapo walijadili masuala mbalimbali kuanzia urafiki wao, siasa, kazi na mengineo.

Mazungumzo yao yalipokuwa yakiendelea, Jalang'o alimuuliza mtumbuizaji huyo kwa nini anamchukia sana. Huku akieleza kuhusu ugomvi wao wa mwaka jana, Kibe alikiri kwamba alisherehekea sana wakati uvumi ulipoibuka katika hatua za awali za kuhesabu kura kuwa mtangazaji huyo wa zamani ameshindwa kunyakua kiti cha ubunge wa Lang'ata kwenye jaribio lake la kwanza 

"Kwanza ukajua vile nilikuchekelea asubuhi vile niliskia umepoteza. Kaka, nilianguka hapa chini. Ungeniona. Nilikuwa nimesherehekea ati Jalas ameishi. Nilikuwa nimekufa,"  Kibe alimwambia mbunge huyo.

Kibe aliweka wazi kuwa alisherehekea uvumi wa kushindwa kwa Jalang'o kwa sababu alikuwa amesema uwongo kumhusu hapo awali.

"Mbona useme maneno kunihusu ambayo sio ya kweli?" Kibe alimuuliza Jalang'o.

Wawili hao walibainisha kwamba hawakuwahi kuzozana katika siku za nyuma na hata walishiriki vinywaji pamoja kama marafiki.

Jalang'o alijitetea kuwa alisema maneno ya uwongo kuhusu mwanapodcast huyo kwa sababu alikuwa amemshambulia pia.

"Kibe wewe ndio ulianza hiyo ufala. Mimi na wewe hatujawahi kukosana. Huwezi kuamka siku moja na kusema maneno yako kwa hizo vitu zako. Ilikuwa ni ugomvi mdogo tu kumbe akaenda ukashika makali," alisema.

Kibe alimkumbusha mbunge huyo wa muhula wa kwanza kuhusu urafiki wao wa muda mrefu na jinsi alivyomtetea katika siku za nyuma wakati aliposhutumiwa kwa kuhusika katika biashara haramu ya 'Wash Wash'.

Wakati mtumbuizaji huyo alipokiri kusherehekea uvumi wa Jalang'o kushindwa kinyang'anyiro cha ubunge wa Lang'ata, mbunge huyo alisema alitazama video yake akifurahiya tetesi hizo na akapuuza tu akitamani pia yeye angekuwa katika kituo cha kuhesabu kura aweze kushuhudia kilichokuwa kikiendelea.