Harmonize atoa masharti makali kwa mapromota kabla ya kukubali kupiga shoo

Pia amewataka mapromota kutenga tiketi zingine nane kwa ajili ya timu na bendi yake.

Muhtasari

• Harmonize amesema ni sharti promota awe tayari kulipa tiketi mbili za eneo la kibiashara katika ndege ili akubali kutumbuiza.

•Ameweka wazi kwa mapromota kuwa mchumba wake hawezi kusafiri katika eneo la uchumi wakati wanapoenda kufanya shoo.

Image: INSTAGRAM// HARMONIZE

Staa wa Bongo Harmonize ametangaza kwamba ni sharti promota awe tayari kulipa tiketi mbili za eneo la kibiashara katika ndege ili akubali kutumbuiza.

Tiketi moja ni yake ilhali nyingine ni kwa ajili ya mchumba wake Kajala Masanja ambaye pia meneja wake.

Harmonize ambaye kwa sasa yupo nchini Qatar kwa ziara ya kikazi pia amewataka mapromota kutenga tiketi zingine nane kwa ajili ya timu na bendi yake.

"Ikiwa huwezi kulipia timu yangu ndege ya kibinafsi, basi hakikisha kuna tiketi mbili za eneo la kibiashara na zingine nane kwa ajili ya timu na bendi yangu," Harmonize alisema kupitia Instastori zake.

Bosi huyo wa Kondegang aliweka wazi kwa mapromota kuwa mchumba wake hawezi kusafiri katika eneo la uchumi wakati wanapoenda kufanya shoo.

"Meneja wangu ni bosi wangu na mke wangu kwa hivyo huwezi kumsafirisha katika eneo la uchumi. Popote ninapoenda, kama hakuna tiketi mbili za eneo la kibiashara, hakuna shoo, ni hayo!" Alisema katika klipu ya video inayomuonyesha akiwa kwa ndege huku Kajala akiwa kando yake.

Konde Boy aliondoka Tanzania siku ya Jumatano kuelekea  Doha, Qatar ambako atakuwa anatumbuiza wikendi hii.

Picha ambazo alipakia Instagram zilionyesha akiwa ameandamana na mchumba wake Kajala pamoja na timu yake.

Wiki iliyopita  Kajala alianza rasmi kazi yake kama CEO wa timu ya usimamizi ya Konde Music Worldwide.

Harmonize alitangaza kuhusu kuanza kazi kwa mchumba wake na kupakia video iliyoonyesha akimsaidia kujiandaa kwa siku yake ya kwanza kazini.

Ukiona nang'aa ujue ni kazi ya mpenzi  wangu @kajalafrida. Anaanza kazi yake rasmi leo," Harmonize aliandika chini ya video ambayo alipakia kwenye Instastori zake.

Mwanamuziki huyo alimteua Kajala kuwa meneja takriban miezi miwili iliyopita baada yao kurudiana.