Mke wangu yupo huru kuniacha - Abel Mutua

Muhtasari

• Mwanafilamu Abel Mutua amesema kwamba mkewe yupo huru kuondoka katika ndoa iwapo atahisi kwamba hapati furaha aliyokuwa akiikusudia.

• Pia amegusia kwamba wapenzi wengi wamerithi tabia hizo kutoka kwa wazazi wao, bila kujua kwamba nyakati zinabadilika na kwamba kuna mambo lazima tuache kuyatumia katika kizazi chetu.

Abel Mutua
Abel Mutua
Image: Instagram KWA HISANI

Mwanafilamu Abel Mutua amesema kwamba mkewe yupo huru kuondoka katika ndoa iwapo atahisi kwamba hapati furaha aliyokuwa akiikusudia.

 Akizungumza na SPM BUZZ, Mutua amesema kwamba anajua hawezi kumfurahisha mkewe, Judy Nyawira milele na hivyo basi yupo huru kutafuta maisha ya furaha kwingine.

Kulingana na Abel ni kwamba watu wengi wapo katika ndoa ila wanaishi maisha ya huzuni kwa sababu wanaogopa kuwapoteza wenzao kwa hofu ya kuanza upya safari ya kimapenzi na wachumba wengine.

Aidha amepinga vikali hulka ya watu kuweka sheria katika ndoa ambazo zinawafunga kutangamana na watu wengine akisema kwamba hatua hiyo inachangia pakubwa wapenzi wengi kutokuwa waaminifu katika ndoa.

Abel Mutua amewaomba mashabiki na wakenya kuzingatia mchakato wa kujijenga binafsi ili kuhakikisha unaishi na raha moyoni kwani utakuwa umeafikia ndoto zako maishani.

Licha ya matamshi hayo, Abel amesema kwamba yeye na mke wake wanaaminiana na kwamba hamna haja ya kujenga mazingira magumu ya kuwa katika ndoa.

Pia amegusia kwamba wapenzi wengi wamerithi tabia hizo kutoka kwa wazazi wao, bila kujua kwamba nyakati zinabadilika na kwamba kuna mambo lazima tuache kuyatumia katika kizazi chetu.