"Tafuta mke uoe!" KRG amchana Andrew Kibe

Muhtasari

• Tafuta mwanamke mzuri umuoe na utapona mzee kuliko kushinda mitandaoni ukiwapotosha vijana kwamba kumhendo mpenzi wako na mapenzi ni kupoteza mali na muda, kitu ambacho ni uongo mtupu - KRG kwa Kibe

KRG the Don na Andrew Kibe
KRG the Don na Andrew Kibe
Image: INSTAGEAM

Wikendi iliyopita, msanii KRG the Don aliamua kuangusha shoka lake la michambo kwa mwanablogu mwenye utata mwingi Andrew Kibe kwa kupakia picha zake za kitambo wakati alikuwa anafurahia matunda ya mapenzi.

Kibe ambaye ana hulka ya kuingilia maisha ya mapenzi ya watu alijipata katika kikaango cha KRG baada ya kujaribu kulizungumzia suala la KRG kutalikiana na mpenziwe.

Hapo ndipo KRG  aliingia kwenye makabrasha yake na kuziachia picha za kitambo za Kibe akiwa amekumbatiana na mwanamke anayedhaniwa kuwa mpenzi wake kipindi hicho na kuamua kutoa wosia kufuatisha picha hiyo.

KRG alimkomesha Kibe kutoingilia mambo ya mapenzi ya watu na kumtaka amtafute mpenzi ili abadilishe hii tabia yake ya kuona baya kwa kila mtu anayefurahia mahaba na mahanjumati na mpenzi wake.

“Yaani kumbe Kibe kwa wakati mmoja alikuwa katika mapenzi moto moto. Sasa naelewa ni kwa nini inauma sana wakati unaona watu wawili wamependana. Ni vizuri utafute mtu umpende kuliko kukashfu mahusiano ya watu wengine. Usichoke kutafuta mapenzi mzee Kibe. Kila mwanaume anahitaji mwanamke mzuri, tafuta mwanamke mzuri umuoe na utapona mzee kuliko kushinda mitandaoni ukiwapotosha vijana kwamba kumhendo mpenzi wako na mapenzi ni kupoteza mali na muda, kitu ambacho ni uongo mtupu,” alitoa wosia KRG.

Msanii huyo hakukomea hapo kwani aliendelea kumchimba Kibe hata zaidi ambapo alipakia picha yake ingine akiwa kanisani na kusema kwamba mtangazaji huyo aliyegeukia uanablogu alikuwa na maisha mazuri sana kabla ya kupitia changamoto za mapenzi zilizombadilisha kabisa mpaka kuwa mkosoaji mkubwa wa mapenzi.