Mimi ndiye bidhaa ya pili kwa ukubwa kusafirishwa kutoka Uganda!- Zari Hassan ajipiga kifua

Muhtasari

•Mama huyo wa watoto watano amedai kwamba baada ya kahawa, yeye ndiye bidhaa nyingine kubwa zaidi kutoka Uganda.

•Hivi majuzi aliandamana na dadake kutembelea kaburi la marehemu mama yao Halima Hassan, na kuweka maua juu yake.

Image: INSTAGRAM// ZARI HASSAN

Kwa sasa mwanasoshalaiti na mwanabiashara mashuhuri Zari Hassan yupo ziarani katika nchi yake ya kuzaliwa Uganda.

Mpenzi huyo wa zamani wa staa wa Bongo, Diamond Platnumz ambaye amekuwa akiendeleza biashara zake Afrika Kusini baada ya kuondoka Tanzania 2018 alitua Uganda mapema mwezi huu.

Kwenye picha na video ambazo amekuwa akipakia Instagram siku za hivi majuzi, Zari ameonekana akibarizi nyumbani kwa babake.

Katika chapisho lake moja, Zari alionekana akiwa kwenye shamba la babake la kahawa. Alifichua kwamba baba yake ni mkulima mkubwa wa kahawa ambaye huwa anaiuza hata nje ya nchi.

"Nipo kwenye shamba la babangu la kahawa. Angalia jinsi kahawa ni mingi,"  Zari alisema kwenye video ambayo alikuwa anaonyesha shamba la babake.

Katika chapisho lingine, mama huyo wa watoto watano alidai kwamba baada ya kahawa, yeye ndiye bidhaa nyingine kubwa zaidi kutoka Uganda.

"Baada ya kahawa, lazima niwe bidhaa ya pili kwa ukubwa kutoka Uganda. Mchuzi wa Uganda," Zari alisema

Zari ametumia ziara yake kuzuru maeneo mbalimbali nyumbani kwao.

Hivi majuzi aliandamana na dadake kutembelea kaburi la marehemu mama yao Halima Hassan, na kuweka maua juu yake.

Mamake Zari alifariki mwaka wa 2017, wiki kadhaa tu baada ya aliyekuwa mumewe, Ivan Semwanga kuaga.