Diamond ajaribu kuigiza, muziki umemlemea - Mwijaku

Muhtasari

• Mwijaku amemshauri Diamond Platnumz kukoma kuimba.

• Alishikilia kwamba umaarufu wake umetokana na ukali wa maproducer wake wala sio uimbaji wake.

Mtangazaji maarufu huko Tanzania, Mwijaku amemtaka msanii Diamond Platnumz kuacha kuimba na kujaribu uigizaji.

Kulingana na Mwijaku, Simba hana kipaji cha kuimba hivyo anapaswa kutafuta unga kwingine.

Mwijaku alisema kwamba umaarufu wa Diamond umesababishwa na maproducer wake ambao wanatoa midundo mikali wala sio ukali wa uimbaji wake.

"...Yule hajui kuimba, labda akajaribu uigizaji," Mwijaku alisema.

Alikuwa akiyazungumza haya alipokuwa akijibu swali katika mahojiano kuhusu Diamond kupewa tuzo ya heshima katika hafla iliyofanyika siku kadhaa zilizopita.

'DC wa Instagram' alishikilia kwamba msanii wa kwanza kabisa kuwahi kupeleka muziki wa Bongo katika soko la kimataifa ni Alikiba wala sio Simba.

Alisema kwamba kipaji cha Alikiba na Harmonize hakiwezi kulinganishwa na cha Diamond Platnumz.

Aidha, alisema kwamba wandani wa Diamond wanaogopa kumwambia ukweli kwamba hajui kuimba kwa kuwa wanalinda riziki yao.

Hili linaonekana kuwa zito mno, Simba atasalimu amri na kuamua kula nyasi ama atazidi kung'ata?