Zuchu kumenyana na Burna Boy katika tuzo za MTV

Hafla ya kutangazwa washindi itafanyika Novemba 13 katika jiji la Dusseldorf nchini Ujerumani.

Muhtasari

• Tanzania simameni juu, msichana wenu ameteuliwa kuwania tuzo za MTV EMA. Mungu ni mwema - Zuchu.

Zuchu ateuliwa kuwania tuzo za MTV EMA
Zuchu ateuliwa kuwania tuzo za MTV EMA
Image: Instagram//zuchu

Jumatano waandaaji wa tuzo za muziki za MTV EMA waliweka wazi orodha ya wasanii watakaowania tuzo hizo za mwaka huu 2022 katika vitengo mbali mbali.

Hafla ya kutangazwa washindi wa tuzo hizo itafanyika Novemba 13 katika jiji la Dusseldorf nchini Ujerumani.

Kilichowafurahisha wengi wa mashabiki wa muziki kutoka ukanda wa Afrika Mashariki ni kwamba jina la msanii Zuchu kutoka lebo ya WCB Wasafi alitajwa pale kumenyana na mastaa mbali mbali katika tuzo hizo ambazo kwa miaka mingi zimekuwa zikitawaliwa na wasanii kutoka Magharibi mwa Afrika.

Zuchu alitajwa kuwania katika kipengele cha Best African Act ambapo atamenyana na wakali wa shughuli hizo kama staa kutoka Nigeria ambaye pia ni mshindi wa tuzo za Grammy, Burna Boy, Black Sherrif kutoka Ghana, Musa Keys kutoka Afrika Kusini, Ayra Starr kutoka Nigeria na Tems kutoka Nigeria pia.

Msanii huyo alidhihirisha furaha yake kupitia kurasa zake kwenye mitandao ya kijamii huku akiwarai mashabiki zake kujibwaga nyuma yake na kumpa shavu kwa kumpigia kura kwa wingi ili kufanikisha tuzo hii kutua nchini Tanzania.

“Tanzania simameni juu, msichana wenu ameteuliwa kuwania tuzo za MTV EMA. Mungu ni mwema, niseme ahsante kwa sababu yenu ndio mimi niko hapa nawapenda sana,” Zuchu aliandika huku akisema kwamba anatetemeka kwa furaha na kuahidi kurejea na maelezo mazuri zaidi.

Msanii Diamond kupitia instastories zake aliipakia picha hiyo akiwaomba mashabiki wake kumuunga mkono Zuchu kwa kumpigia kura huku akisema kwamba macho yake yanaona Zuchu akatwaa huu ubingwa.

“Macho yenu yanaona kama ninavyoona mimi lakini au,” Diamond aliandika.