Zuchu ateuliwa kutumbuiza AFRIMMA siku chache kabla ya kuteuliwa kwenye tuzo za MTV

Kando na kutumbuiza, pia atakuwa anawania tuzo katika kitengo cha Best Female East Africa.

Muhtasari

• Afrimma vile vile waliweka wazi kwamba Zuchu ameteuliwa kuwania tuzo hizo katika kitengo cha Best Female East Africa.

Zuchu ateuliwa mtumbuizaji rasmi AFRIMMA
Zuchu ateuliwa mtumbuizaji rasmi AFRIMMA
Image: Instagram

Malkia wa muziki kutoka Zanzibar, Zuchu anazidi kuzikwea ngazi za mafanikio katika muziki si tu katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bali pia katika janibu zote kwenye tasnia ya muziki duniani.

Siku chache tu baada ya kuteuliwa kuwania tuzo maarufu za MTV EMA katika kitengo cha Best African Act, msanii huyo tena ameteuliwa kama mtumbuizaji maalum katika tuzo za Afrimma za mwaka huu.

Tuzo za Afrimma zitafanyika katika jiji la Dallas, Texas nchini Marekani mnamo tarehe 19 mwezi Novemba.

Kupitia ukurasa wao rasmi wa Instagram, Afrimma walipakia video ya kudensi ya Zuchu akicheza wimbo wake mpya wa Kwikwi pamoja na wacheza densi wake na kusema kwamba ni rasmi msanii huyo atakuwa miongoni mwa watumbuizaji watakaopamba sherehe hizo.

Afrimma vile vile waliweka wazi kwamba kando na msanii huyo kuteuliwa kama mtumbuizaji, pia ameteuliwa kuwania tuzo hizo katika kitengo cha Best Female East Africa.

“Zuchu atatumbuiza moja kwa moja kwenye Onyesho la TUZO ZA AFRIMMA mwaka huu. Zuchu ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo kutoka Tanzania mzaliwa wa Zanzibar lakini mwenye makazi yake jijini Dar es Salaam. Ameteuliwa katika kitengo cha "BEST FEMALE EAST AFRICA" kwa tuzo za mwaka huu. AFRIMMA 2022 itakuwa imejaa pomoni na mastaa watakaofurika ukumbini. Usifungiwe nje!” Afrimma waliandika kwenye video hiyo.

Kama msanii huyo atafanikiwa kuzitwaa tuzo za Afrimma na pia MTV EMA basi huu utakuwa mwaka wa kipekee kwake kwani itakuwa kama amewinda ndege wawili kwa jiwe moja na kufanikiwa kuwanasa.

Kila la Kheri Zuchu!