Namuogopa sana mpenzi wangu, nazima simu yangu akiwa karibu - Akothee

Mwanamuziki huyo alimpokea Bw Schweizer aliporejea nchini baada ya wiki mbili na ushee

Muhtasari

• Mwanamuziki huyo alisema kuwa licha ya mpenzi wake kuwa mtu mwenye umakini, ni mwenye upendo na mnyenyekevu.

• Akothee alisema kuwa Bw Schweizer humfanya awe mtu mtulivu.

Akothee na mpenzi wake

Mwanamuziki Akothee amesema kuwa mpenzi wake Bw Schweizer humpa woga kwa kuwa na ukali wakati mwingine.

Katika ukurasa wake wa Instagram, Akothee alimwandikia mpenzi huyo wake ujumbe ulioonyesha anavyothamini uhusiano wao.

Alisema kuwa ilibidi ajue kuwa mtulivu na mwenye heshima kwa mpenzi huyo wake aliyembandika jina la Omondi.

Aliongeza kuwa licha ya Bw Schweizer kumwonyesha mahaba na kuwa mwenye upole, ni mtu aliye na umakini kwa mambo yake.

"Mimi humuogopa Omosh, ni mkali. Akisema niache ninachofanya, mimi hujikunja kama jongoo," mwanamuziki huyo alisema.

Hata hivyo, Akothee bado alimwonyesha mpenzi huyo wake jinsi anavyompenda katika ujumbe huo wake.

Alisimulia jinsi mpenzi wake ni mtu aliye na mahaba na mwenye urafiki kwake kando na kuwa mtu mwenye umakini mno.

"Nilikutana na mtu mnyenyekevu, mwenye upendo ila ni mwenye umakini sana.  Mjue kwamba simu zangu huzimwa kutoka saa kumi na mbili jioni wakati Bw Omosh ako karibu nami," mama huyo aliwafahamisha rafiki zake.

Akothee alikuwa ametangaza kuwa amekuwa akisubiria mpenzi wake kurejea nchini kwa muda sasa.

Katika picha hiyo aliyopakia kwenye ukurasa wake, alionekana kumkumbatia mpenzi huyo wake mzungu kwa mahaba.

Alikuwa amesema alivyompeza Bw Schweizer alivyokuwa hayuko nchini na hata kuwa na hamu ya kumpokea.

Siku  ya Jumatano, Akothee alikuwa amesema jinsi kukaa siku chache mbali na mpenzi wake kulimpa upweke.

"Bi Omosh, tayari kumpokea Omosh, mpenzi nimekupeza sana. Siku hizo 16 zilihisi kama mwaka. Kuja twende Rongo. Nakupenda sana," mwanamuziki huyo alimwandikia 'Omosh' ".