Diamond Platnumz abubujikwa na furaha baada ya Radio Jambo kupakia wimbo wake

Msanii huyo alipakia kionjo cha wimbo wake ambao Radio Jambo walikuwa wameweka mitandaoni na kutoa shukrani zake.

Muhtasari

• Msanii huyo aliihongera Radio Hii kwa kueneza muziki wake na kuufanya kuwa namba moja kaktika jukwaa la Boomplay nchini Kenya.

Diamond aonesha furaha yake Radio Jambo wakipakia wimbo wake
Diamond aonesha furaha yake Radio Jambo wakipakia wimbo wake
Image: Instagram

Msanii namba moja katika ukanda wa Afrika Mashariki kwa miziki ya kizazi kipya Diamond Platnumz ameonesha kufurahishwa kwake baada ya kituo cha Radio Jambo kupakia kionjo cha video yake kwenye ukurasa wa Instagram.

Radio Jambo walipakia kionjo cha msanii huyo kwenye mitandao ya kijamii katika kipengele cha ‘Video ya Siku’ – wimbo mpya wa ‘Yatapita’ ambao umetoka siku mbili zilizopita.

Diamond aliiona video ile na kuichukua ambapo pia aliipakia kwenye Instastory yake. Alishukuru Radio Jambo kwa kuendelea kumpa shavu muda wote na kuhakikisha kuwa wimbo huo wake unazidi kukwea ngazi na kuteka mawimbi ya humu nchini.

Mpaka sasa, wimbo huo unazidi kushikilia usukani katika mtandao wa Boomplay wa nchini Kenya kama wimbo ambao umefuatiliwa pakubwa tangu atoe video yake siku ya Jumanne.

Image: Instagram

Ikumbukwe msanii huyo namba moja wa muda wote katika ukanda huu mwenye jina la majazi la Simba alitoa ahadi kwa mashabiki wake kuwa mwaka huu ameiweka rehani mahususi kwa kuwaburudisha tu, huku akisema wale wote ambao wamekuwa wakimsema kuwa simba kapoteza makali wataula wa chuya mwaka huu.

Alikula yamini kuwa mwaka huu ukanda wa Afrika Mashariki utajivunia kuwa na msanii kama yeye kwani amejitoa mazima kuipeperusha bendera ndani na nje ya bara la Afrika.

Diamond aliwatania mashabiki wake kuwa atatoa nyimbo za aina yote huku akiwatayarisha kifikira na kimawazo kuwa wasije wakashangaa watakapomsikia ameimba mpaka kwa lugha za kigeni kama Kichina.