Edday Nderitu aumizwa na vitendo vya Samidoh kutoka kimapenzi na Karen Nyamu

"Nilikupa mapenzi, lakini ulinipa uchungu. Nilikuwa mzuri kwako, ukawa mbaya kwangu.Ulinipa kuzimu wakati nilikupa neema…" - Nderitu.

Muhtasari

• Mama huyo alionesha kwa hisia jinsi Samidoh amekuwa akimuumiza katika suala la mapenzi kwa muda.

Edday Nderitu apakia video ya kuelezea hisia za kuvunjwa moyo
Edday Nderitu apakia video ya kuelezea hisia za kuvunjwa moyo
Image: Instagram, Maktaba

Wakati mwingine mtu anapozidiwa na hisia hadi kushindwa kuzungumza, hutumia video au nyimbo kuwasilisha ujumbe wake!

Edday Nderitu, mpenzi wa mwanamuziki Samidoh anaonekana katika siku za hivi karibuni kulemewa na athari za kuvunjwa moyo na mume wake.

Samidoh hata baada ya kukiri kumkosea Nderitu na kuomba msamaha wa hadharani mwakac 2021, lakini bado alirudi kwenye penzi la Karen Nyamu kwa mara nyingine tena n ahata kupata mtoto wa pili na seneta huyo.

Muda wote huu, Nderitu amekuwa akionekana kumtetea na kumtakasa mume wake Samidoh kwenye mitandao ya kijamii, lakini sasa ni kama kikombe chake kimejaa na kimepwa.

Kama kile amabcho amekuwa akipakia kwenye instastories zake katika siku za hivi karibuni ni kitu cha kuamini, basi hatutakuwa tunakosea tukisema kuwa Nderitu anapitia wakati mgumu sana wa kumbukumbu za Samidoh kumsaliti kimapenzi na Nyamu.

Jumamosi jioni, Nderitu alipakia video ya kuelezea jinsi mtu anahisi akimzomea mpenzi wake baada ya kumdhalilisha kwa kuchepuka na wapenzi wa pembeni.

“Nilikuwa mzuri kwako, lakini wewe ulikuwa mbaya kwangu. Mimi nilikuwa ardhi imara kwako, lakini wewe ukawa mbavu dhaifu. Nilikupa mapenzi, lakini ulinipa uchungu. Ulinipa kuzimu wakati nilikupa neema…” sehemu ya maneno kwenye video hiyo yalikariri.

Video hiyo ilizidi kusimulia kwa uchungu jinsi mapenzi yalimfanya mhusika kujiona mtu asiye na thamani kwani kile alichokipata kutoka kwa mwenzake ni kinyume cha kile alichojitolea kwake.

“Nilikuwa mzuri kwako, ukawa mbaya kwangu,” Video hiyo ilizidi kukariri.

Edday Nderitu kwa muda mrefu amesimama upande wa mume wake Samidoh licha ya kudhalilishwa na vitendo vyake, kitendo cha aibu cha hivi karibuni kikiwa cha Desemba mwaka jana kule Dubai ambapo alilazimika kushusha timbwiri dhidi ya Karen Nyamu wakimpigania mume wake hadharani kwenye ukumbi uliojawa mamia ya mashabiki.

Samidoh alikuwa ukumbini taayri kutumbuiza wakati Nyamu alifika pale na kutembwereka kwenye mapaja ya msanii huyo, jambo lililomghasi Nderitu aliyefika kwa kasi ya duma na kujaribu kumuondoa Nyamu kutoka kwa paja la mume wake, na hapo pakachanika wanawake hao wawili wakimpigania mwanamume huyo aliyesimama kando macho yakiwa yamemtoka pima kama mlevi aliyepigwa mwanga mkali wa tochi usiku gizani kwa ghafla.