Produsa Bob Junior akanusha kufa, kufuatia kifo cha simba 'Bob Junior' mbugani Serengeti

Simba Bob Junior alifariki na wengi wakadhani ni msanii Bob Junior, ambaye pia ni produsa katika lebo ya Sharobaro Empire.

Muhtasari

• Simba Bob Junior alifariki Machi 11 baada ya kushambuliwa na kundi la simba watatu waliokuwa na njama ya kupindua utawala wake porini Serengeti.

Msanii Bob Junior akanusha kufa, kifo chake chachanganywa na cha simba
Msanii Bob Junior akanusha kufa, kifo chake chachanganywa na cha simba
Image: Instagram, BBC NEWS.

Mzalishaji wa muziki na mmiliki wa lebo ya Sharobaro Music Empire Bob Junior amejitokeza na kuweka wazi kwamab ameona taarifa nyingi mitandaoni watu wakimuomboleza kuwa amefariki dunia.

Hii ni kufuatia taarifa za mamlaka ya wanyamapori kutoka mbuga ya Serengeti kusema kwamab simba mkongwe Zaidi katika mbuga hiyo kwa jina Bob Junior alifariki dunia baada ya kushambuliwa na wenzake ambao walikuwa wanataka kuchukua uongozi wake mbugani.

Mhifadhi Mwandamizi wa hifadhi hiyo, Fredy Shirima aliieleza BBC kuwa kundi la simba watatu ambao walikuwa kwa muda mrefu na njama ya kutengua utawala wa simba Bob Junior ndio walimshambulia na kumuua.

“Bob Junior aliuawa siku ya Machi 11, akishambuliwa na Simba watatu ambao walikuwa sehemu ya kundi la simba saba waliokuwa wanapanga mapinduzi. Kwa kawaida hatuwezi kuingilia maisha ya wanyama pori… hivyo kilichotokea kilipangwa miongoni mwao ikiwa ni vita vya kimapinduzi na simba huwa wana tabia hiyo ambapo mtawala anapozeeka hutolewa kimabavu,” alieleza.

 

 Kufuatia taarifa hizo, watu walidhani ni msanii Bob Junior aliyefariki na bila kuhakiki kwa masikio yao, walifurika mitandoani kumuombea dua ya kupumzika pahali pema palipo wema msanii huyo.

 

Hata hivyo, msanii huyo amejitokeza wazi na kuvunja ukimya wake akisema kwamba si yeye bali ni mnyama simba, akiwataka watu kufanya uhakiki kabla ya kuapagawa mitandaoni.

 

“Nimepokea simu nyingi kutoka kwa watu mbalimbali kufuatia kifo cha 'Bob Junior' wengi wameshituka wakijua ni mimi, kwa upande wangu mimi ni mzima wa Afya na niwaondoe watu hofu juu ya hili wasiwe na wasiwasi kuhusu mimi, pia nawapa pole waliofiwa na kuguswa na kifo cha Simba 'Bob Junior’” Alisema.