Andrew Kibe: Niko tayari kumlipa Thee Pluto kama atakubali kufanya DNA na mwanawe

Kibe alisema haya siku chache baada ya Pluto kudokeza kwamba anapambana na tatizo la msongo wa mawazo bila kusema kinqachomsababishia tatizo hilo.

Muhtasari

• "Acha niiweke hivi, nitakupa dola elfu moja kufanya DNA na pia nitakupa dola zingine elfu moja kwa kukubali tu kufanya DNA,” Kibe alimwambia.

Andrew Kibe amtaka Thee Pluto kufanya DNA.
Andrew Kibe amtaka Thee Pluto kufanya DNA.
Image: Screengrab//Andrew Kibe YouTube.

Siku chache tu baada ya Thee Pluto kubainisha wazi kwamba anaugua kutokana na msongo wa mawazo na kuwataka mashabiki wake kumuombea, mwanablogu Andrew Kibe amedokeza kuwa huenda tatizo hilo ni kutokana na dhana kwamba hajui kama ni baba kweli kwa mtoto Zoey.

Kibe katika podikasti yake ya Jumatatu, alisema kuwa safari hii yuko tayari kumlipa Thee Pluto kiasi cha dola za Kimarekani elfu moja sawa na elfu 135 za Kenya endapo atakubali kufanya DNA na mwanawe Zoey na tukio hilo lirekodiwe naye.

“Thee Pluto kama unasikiliza, niko tayari kufanya hiyo DNA. Acha niiweke hivi, nitakupa dola elfu moja kufanya DNA na pia nitakupa dola zingine elfu moja kwa kukubali tu kufanya DNA,” Kibe alimwambia.

Alimtaka Pluto kukumbatia fursa hiyo na kupata dola elfu moja chini ya dakika kumi ambazo zoezi hilo litachukua.

“Tunakubaliana tu kufanya DNA, kama matokeo yatakuwa chanya au hasi hilo sijui. Mimi nitalipia DNA na pia nitakupa dola elfu moja kwa kukubali kufanya DNA. Na kit utu unahitajika kufanya ni kuketi pale, hata huhitaji kusema chochote, halafu mtu wangu atakurekodi,” Kibe alimwambia Pluto.

Hii si mara ya kwanza kwa Kibe kumtaka Pluto kufanya DNA kwani mwishoni mwa mwaka jana Felicity Shiru, mpenzi wa Thee Pluto alipozaa, mwanablogu huyo alikuwa wa kwanza kumsisitizia umuhimu wa kufanya DNA akiashiria kwamba huenda mtoto huyo si wake.