Cebbie Koks ausaliti undungu na Akothee, apanda mbegu ya urafiki kwa 'adui' Zari Hassan

Licha ya Akothee kuwa na bifu na Zari Hassan, Cebbie Koks hakutaka kuipa uhai falsafa ya "damu ni nzito kuliko maji" na alionsha kumkubali Zari.

Muhtasari

• Zari alipakia sasisho akiwausia watu kujikubali kwanza kabla ya kuwapa vipaumbele watu wengine.

• Cebbie Koks alimmwagia makopa kopa na kumtaja kama malkia.

Cebbie Koks aonesha urafiki mkubwa na Zari Hassan, mbaya wa dadake Akothee.
Cebbie Koks aonesha urafiki mkubwa na Zari Hassan, mbaya wa dadake Akothee.
Image: Instagram

Uhasama baina ya dada wa toka nitoke kutoka tumbo moja Cebbie Koks na Akothee hauko karibu na kupata ufumbuzi kabisa.

Wawili hao wamekuwa wakitupiana vijembe mitandaoni na hata kuoneshana wazi wazi kwamba hawawezi pikwa kwenye chungu kimoja wakapikika, chanzo kikiwa ni chuki ya mafanikio, kulingana na Akothee.

Kwa muda mrefu wanamitandao wamekuwa wakifahamu kwamba Akothee na mfanyibiashara kutoka Uganda, Zari Hassan wamekuwa na bifu ambalo halijui chanzo chake ni kipi.

Sasa dadake Akothee Cebbie Koks ametumia fursa hii kumfuma Akothee mkuki wa moja kwa moja kwa kuonesha upendo wake kwa Zari huku akimuita Malkia, jambo ambalo limeonekana kama ni kumtumia ujumbe dadake kuwa Zari ndio ‘madam boss’ wa kweli na wala si yeye.

Zari alipakia picha kwenye Instagram yake akiwashauri mashabiki wake kujipa kipaumbele katika kila kitu wanafanya na wala si kuwapa watu wengine vipaumbele.

Hapo ndipo dadake Akothee Cebbie Koks aliwahi kwa haraka na kukumwagia makopa akimtaja kama malkia na kuweka emoji za mapenzi.

Zari naye kwa kuzidisha kolezo la chumvi alimjibu Koks kwa emoji za mapenzi kuonesha kuwa amemkubali.

Hili liliwaacha wengi katika gumzo pevu wakisema kuwa Koks alikuwa anataka kumuonesha dadake hadharani kuwa hawezi mkubali na badala yake kuamua kumpa maua mbaya wa dadake.

Katika siku za hivi karibuni, Zari na Akothee ambao wana vitu vingi vinavyowafananisha kutoka umri, maisha yao ya mahusiano, idadi ya watoto na kibiashara wamekuwa wakionesha kama wanashindana hivi, kila mmoja akijaribu kuonesha kuwa ndiye malkia wa mitikasi katika ukanda wa Afrika Mashariki.

Baada ya Akothee kufunga harusi iliyomfanya kutrend mitandaoni kwa Zaidi ya wiki moja, saa 48 baadae Zari naye alifunga harusi ya Nikkah na mpenzi wake mdogo Shakib Cham, kuwafanya watu waibue mjadala kwamba yeye na Akothee walikuwa wanashindana.