"Kwetu, haukuwa kuhusu uchaguzi!" Gidi Gidi afichua sababu halisi kwa nini walitunga wimbo 'Unbwogable'

Gidi amefunguka kuhusu wimbo wao maarufu ‘Unbwogable’ ambao waliimba zaidi ya miongo miwili iliyopita.

Muhtasari

•Gidi amefichua kuwa masaibu mengi ya maisha yalimsukuma yeye na Maji Maji kufanya wimbo huo ambao ulivuma sana Afrika nzima.

•Alisema wakati huo alikuwa katika chuo kikuu kwa sasa na yeye na Maji Maji walikuwa hawajafanikiwa kutengeneza pesa licha ya bidii yao katika muziki.

Mtangazaji Gidi Ogidi
Image: RADIO JAMBO

Mtangazaji wa Radio Jambo, na ambaye ni mwanamuziki wa zamani,  Joseph Ogidi almaarufu Gidi Gidi amefunguka kuhusu wimbo wao maarufu ‘Unbwogable’ ambao waliimba zaidi ya miongo miwili iliyopita.

Wimbo huo ambao alilimba pamoja na mwenzake wa kundi la Gidi Gidi Maji Maji, Julius Owino almaarufu Maji Maji ulihusishwa sana na siasa, jambo ambalo mtangazaji huyo wa kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi kwenye Radio Jambo sasa amezungumzia ili kuweka mambo wazi.

"Unbwogable ilifanywa mwaka wa 2002, wakati wa uchaguzi wa 2002. Watu wengi wanauhusisha na uchaguzi wa wakati huo, ingawa kwetu haukuwa kuhusu uchaguzi," Gidi alisema katika mahojiano na KTN Home.

Mwanamuziki huyo wa zamani alifichua kuwa masaibu mengi ya maisha yalimsukuma yeye na Maji Maji kufanya wimbo huo ambao ulivuma sana Afrika nzima.

Alisema wakati huo alikuwa katika chuo kikuu kwa sasa na yeye na Maji Maji walikuwa hawajafanikiwa kutengeneza pesa licha ya bidii yao katika muziki.

“Nilikuwa katika chuo kikuu cha KCA. Maji Maji alikuja na kuniuliza “tutafanyaje sasa? Tumetoka tu kutengeneza albamu na bado hatupati pesa”.

Mimi nilikuwa nimeamua kurudi chuo na kuendelea na elimu yangu, kwa kweli nilikuwa tayari nimekata tamaa na kusema sitaki tena kufanya muziki.

Lakini Maji Maji alikuwa akiniambia ‘tufanye tu’. Kisha nikamwambia Maji, nadhani tuko Unbwogable. Mimi ni unbwogable. ilikuwa zaidi kujipa motisha,” alisema.

Bwogo ni neno la Kijaluo lenye maana ya ‘kutisha’, kwa hiyo ‘Unbwogable’ ilikusudiwa kumaanisha ‘huwezi kunitisha’

Gidi aidha alisherehekea kuwa wimbo huo walioufanya ili kujipa motisha ulivuma sana hadi hata wanasiasa wakauchukua kwa matumizi yao ya kisiasa.

"Wanasiasa waliuruki.. Ulichezwa katika vituo vyote vya redio. Kuna hadithi nyingi kuhusu wimbo huo ambazo siwezi hata kuzielezea,” alisema.

Mwimbaji huyo wa zamani pia alisema wimbo huo uliwapa heshima kubwa hata katika tasnia ya muziki duniani, akifichua kuwa hata walipigiwa simu na kampuni ya kimataifa ya muziki, Galo Records, ambayo ilizungumza nao kuhusu jinsi Muziki wa Mjini wa Afrika ulivyokuwa ukikaribia kuvuma.