"Zuchu anachumbiana na Diamond, nilimkuta kwake akimtengea chakula" - Baba Levo

Baba Levo alitoa sababu nyingi za kuonesha kwamba Diamond na Zuchu ni kitu kimoja.

Muhtasari

• Baba Levo alisema wawili hao hawaweki mambo wazi na wamewaacha wengi katika hali ya kutojua ukweli .

Msanii baba Levo na Diamond na Zuchu
Msanii baba Levo na Diamond na Zuchu
Image: Instagram

Msanii Baba Levo ameibua sababu kadhaa za kufanya watu wasadiki kwamba  Zuchu na bosi wake msanii Diamond Platnumz wapo kwenye mahusiano ya kimapenzi.

Akizungumza katika kituo cha redio cha Wasafi FM, Baba Levo alielezea kwamba kulingana na anavyoona mastaa hao wawili wakifanya mambo yao, ni wazi kwamba wao ni kitu kimoja.

“Zuchu kwa mimi ninavyoona yuko kwenye mahusiano na Diamond Platnumz na hii ni kwa maono yangu na nitatoa sababu. Nimeenda kwa Diamond nimemkuta Zuchu anamtengea Diamond chakula wakati huo Diamond anaye dada wa nyumbani kule, dada zake kina Esma wapo lakini Zuchu ndio anamtengea chakula, alieleza Baba Levo.

Akielezea sababu zaidi za kumfanya aamini kuwa wawili hao wapo kwenye mahusiano, Baba Levo alisema kwamba wakati mwingine Zuchu hata alikuwa anamlisha Diamond baada ya kumwandalia.

“Muda mwingine, Diamond ana sebule tatu, kuna hiyo sebule moja ambayo hatukanyagi sisi, awe Mbosso, Rayvanny, nani, hawakanyagi, lakini utamkuta Zuchu mule,” Baba Levo alizidi kutetea kauli yake kwamba Zuchu wanachumbiana na Diamond Platnumz.

Baba Levo alipoulizwa ikiwa Diamond mwenyewe ashawahi kumwambia wazi kama kweli yupo kwenye mahusiano na Zuchu kutokana na ukaribu wao, alisema kwamba amejaribu mara kadhaa kumbana bosi huyo wa WCB na ambapo anakaribia kusema lakini anaishia njiani tu na kusema kwamba wote wapo vuguvugu tu wameacha kila mtu katika njia panda.

Pia msanii huyo chawa wa Diamond alimtaka Zuchu kuweka wazi kama kweli wanachumbiana na Diamond.

“Tuambieni Zuchu, mahusiano si kitu kibaya, Diamond si kwamba ni mtu mwenye sura mbaya tuseme ukiwa unachumbiana naye watu watakucheka uonekane kama ni mtu wa hovyo,” Baba Levo alimsisitizia Zuchu.

Baba Levo alizidi kutoa sababu za kuwepo kwa mahusiano ya Diamond na Zuchu ambapo pia alisema siku hizi mtu akitaka kupata hela kwa Diamond kirahisi ni sharti apitie kwa mwanadada Zuchu.