Coronavirus: Afisa aliyetemewa mate na mtu mwenye Covid-19 aaga dunia

Afisa anayekatisha tiketi amefariki baada ya kutemewa mate na mwanaume mmoja anayedaiwa kuwa alikuwa na maambukizi ya virusi vya Covid-19.

Belly Mujinga, 47, ambaye alikuwa na matatizo ya kupumua, alikuwa akifanya kazi katika kituo cha Victoria jijini London mwezi Machi alipodhalilishwa, sambamba na mfanyakazi mwenzie wa kike.Ndani ya siku kadhaa baada ya tukio hilo, wanawake wote waliugua ugonjwa wa Covid-19. Polisi wamesema kuwa madai yamefunguliwa ili kumtafuta mwanaume aliyeatemea mate wanawake hao wawili.

Bi. Mujinga alikuwa kwenye kituo hicho tarehe 22 mwezi Machi wakati alipokabiliwa na mshukiwa huyo. Mumewe Lusamba Gode Katalay alisema mwanaume huyo alimuuliza mke wake alikuwa akifanya nini pale.

''Alimjibu alikuwa kazini pale na mtu huyo akasema ana virusi kisha akamtemea mate,'' aliongeza.

Bibi Mujinga alilazwa hospitali ya Barnet tarehe 2 mwezi Aprili na kuwekwa kwenye mashine ya msaada wa kupumua. Lakini alifariki siku tatu baadae, Shirikisho la wafanyakazi wa usafirishaji (TSSA) lilisema.

Msemaji wa ofisi ya Waziri Mkuu amelielezea shambulio hilo dhidi ya mfanyakazi wao muhimu ni ''la dharau''

Bwana Katalay alisema alimpigia simu mkewe kwenye programu ya video alipokuwa hospitalini, lakini hakusikia kutoka kwake tena.

"Nilidhani anaweza kuwa amelala, lakini daktari alinipigia simu kuniambia kuwa amefariki," alisema.

"Alikuwa mtu mzuri, mama mzuri, na mke mzuri. Alikuwa mtu anayejali na angemtunza kila mtu."

Watu kumi walihudhuria mazishi ya Bi Mujinga, pamoja na binti yake wa miaka 11.

Binamu yake Agnes Ntumba alisema  kuwa Bi Mujinga anaamini yuko salama katika mazingira yake ya kawaida ya kazi .

"Haipaswi kumfanya afanye kazi kwenye msongamano huo," alisema.

"Hangekuwa amekufa katika hali hii. Tungeweza kuyazuia - ikiwa angekuwa na PPE zaidi au ikiwa wangemweka ndani badala ya kuwa kwenye sehemu ya wazi''.