Divorce:Chunga! Sababu 8 ambazo zinaweza kuvunja ndoa yako

together
together
Siku hizi kuingia na kuondoka katika ndoa ni kama mchezo wa  ‘cha baba na cha mama’. Hakuna wanaoipa ndoa heshima na hadhi yake kama ilivyokuwa hapo awali .Ndoa  thabiti ndio msingi wa jamii endelevu na ishara ya ustawi wa kizazi kijacho .Msukosuko katika ndoa ni ishara ya ukosefu wa msingi katika hatua ya kwanza ya kujenga taifa au jamii yenye mtazamo wa kujenga kikubwa cha kudumu .Je,Mbona kuna talaka nyingi siku hizi? Sababu ndio hizi .. na kuna nyingi zaidi ambazo hazimo katika orodha hii

1.  Kutojitolea/kukosa kuaminiana

Ingawaje nguzo muhimu ya ndoa ni mtu kujitolea kuwa na mwenzake kwa mbivu na mbichi  idadi kubwa ya watu hawajajituma katika ndoa zao na baada ya miaka miwili utepetevu unaanza kuingia katika uhusiano wenu na kila mtu anakosa kumjali mwenzake . Hatua hii hufanya ndoa kukosa mvuto na baadaye kusababisha watu kutaka  kutalakiana

2.  Usinzi /mahusiano ya nje ya ndoa

‘Mipango ya kando’ ni mojawapo ya sababu kuu ambazo huwafanya watu kutalakiana . Endapo mwenzako atagundua kwamba unakula tunda  jingine na sio lake tu basi ole wako! Safari ya talaka imeanza . Unapoanza kuwa na mahusiano ya nje ya ndoa mwenzako huhisi kutengwa , na pia kupatwa na hofu ya uwezekano wa kuachwa .Wakati huo watu wengi huwa na chaguo la kujiondoa  mapema kutoka ndoa hiyo kuliko kungoja hadi watakapoachwa .

3.  Migogoro na malumbano ya mara kwa mara .

Kuna haja ya wanandoa kutafuta  jinsi ya kusuluhisha mizozo yao  na pia kupunguza malumbano ambayo yana hatari ya kuvuruga uhusiano wao . ishara za mwanzo kwamba chuma kitaingia  moto ni ugomvi na kelele  kati yenu .mmoja wenu baadaye huchoka na kelele hizo na baadaye kuamua kwamba  anataka kuondoka .

4.  Kuolewa au  kuoa ukiwa na umri mdogo .

Wengi  wa wanandoa ambao wana jumla ya umri wa miaka 23.3 wapo katika uwezekano wa juu kutalakiana . ingawaje kumekuwa na  ongezeko la umri wa mtu kuoa au kuolewa hadi miaka 50,ndoa za watu walio na umri mdogo zimepatikana kuwa na matatizo si haba . Mnapooana mkiwa wadogo ndivyo ilivyo hatari ya ndoa yenu  kuvunjika haraka ikilinganishwa na wale waliofunga pingu za maisha wakiwa na umri wa juu kidogo .

5.  Matatizo ya Kifedha

Utafiti umeonyesha kwamba ukosefu wa fedha za kuendesha mipango yenu kama wanandoa ni hatua inayoweza kusababisha talaka .wakati pesa zinapokosekana kuna uwezekano wa kuwepo hali ya taharuki  ambayo pia huvuruga uhusiano wenu .Kila mmoja wenu ana mawazo kuhusu mtakavyogharamia hiki na kile na hivyo basi hamna muda wa kuzungumza mambo yanayohusiana   nanyi .Kwa kinaya , pesa nyingi nazo zina uwezo wa kusababisha matatizo katika ndoa pia .Iwapo hamtajua  au hamna mpango wa kuzitumia pesa zenu hasa katika hali ambapo hamukua na pesa hapo awali –basi kuna mmoja au  nyote mtabadilika kwa njia mbaya itakayovuruga ndoa yenu .

6.  Kutumia dawa za kulevya/mihadarati

 

Takriban asilimia 30 ya wana ndoa wa zamani wametaja utumizi wa mihadarati kama sababu iliyowafanya kutalakiana . ulevi kupindukia ,sigara ,bangi na dawa za kulevya kama vile cocaine na  mandrax husababisha msukosuko katika uhusiano wowote na ndoa haijasazwa katika patashika za matumizi ya mihadarati .kama sio pesa za kununua dawa hizo basi ni matokeo ya kuzitumia kama vile kuvurugana au kusahau kufanya jambo au kulifanya kwa njia isiofaa .

7.  Dhulma za kupigwa/kuvurugwa kiakili

 Takriban robo ya ndoa zote zinazovunjika hutokana na dhulma za  mmoja dhidi ya mwenzake .dhulma  hizo sio lazima ziwe za mtu kushambuliwa bali pia kukukwazwa kimawazo au hata kukufanya uwe na mawazo kupindukia . kuwa katika hali tete ya kifikra ni jambo  linaloweza kukufanya ujichukie na uamue hata kujiua . watu wengi huvumilia kwa muda  lakini dhulma katika ndoa zina hatari na hivyo basi wengi huamua kupata talaka kabla ya mambo hayajachacha .

  1. Muingilio wa kifamilia na marafiki

 Kuna Ndoa ambazo huvunjika kwa sababu ya muingilio wa jamaa kutoka pande zote .Tofauti kati ya mmoja wenu katika ndoa na jamaa za mwingine huweza kukomaa na kuwa kidonda kikubwa katika ndoa yenu .Hatimaye mwenzake  huhisi kana kwamba hufanyi chochote kumkinga dhidi ya jamaa zako na kuamua kupata talaka .  Unafiki wa marafiki na jamaa zenu pia ni jambo mnalofaa kuwa makini nalo.Kuamini kila unachoambia na huyu na Yule bila ithibati ni mambo hatari katika ndoa .Wakati weote hakikisha  unaikinga imani ya mwenzako katika kila unalosema na kufanya .