Kocha wa timu ya taifa ya wanawake Beldine Odemba amesafiri na kikosi chake cha Harambee Starlets kuelekea Antalya, Uturuki.
Timu hiyo imeratibiwa kushiriki katika kipute cha Pink Ladies kitakachofanyika nchini Uturuki kuanzia Jumanne 22 mwezi huu na kukamilika tarehe 31 Oktoba.
Harambee Starlets, iliondoka nchini Jumatatu tarehe 21 na imeratibiwa kucheza mechi tatu dhidi ya wapinzani waliojisajili kucheza mashindano hayo ya Pink Ladies.
Mnamo Septemba 23, Timu hiyo ya Kenya itacheza dhidi ya Chinese Taipei mwendo wa saa 10 jioni mechi ya kwanza. Mechi ya pili, itachezwa mwendo wa saa moja usiku tarehe 26 Oktoba dhidi ya Russia kabla ya kucheza mechi ya mwisho mnamo Jumatano tarehe 30 dhidi ya Phillipines saa 10 jioni.
Katika kushiriki kwa Harambee Starlets, fursa hiyo inalenga kuimarisha kikosi cha kocha Beldine Odemba kwa mashindano ya mbeleni pamoja na wachezaji kuonyesha vipaji vyao katika rubaa za kimataifa.
Kocha Odemba ameondoka na kikosi cha wachezaji 21 kikiwemo walinda lango wawilli Annedy Kundu na Judith Osimbo.
Mabeki ni Fanis Kwamboka, Vivian Nasaka, Mollyne Akinyi, Ruth Ingosi, Norah Ann, Lavender Akinyi na Wincate Kaari.
Providence Khasiala, Lydia Akoth, Lorna Nyarinda, Robby Maximilla na Fasila Adhiambo ndio watacheza katika safu ya kati huku washambulizi wakiwa Ann Arusi, Rebecca Okwaro, Lucy Kwekwe, Elizabeth Mutukiza, Purity Alukwe pamoja na Beverlyne Achieng.