Gavana wa Garrissa Ali Korane kufikishwa mahakamani leo Jumanne baada ya kulala korokoroni

Gavana wa Garissa Ali Korane  anatarajiwa kufikishwa makamani leo Jumanne kujibu mashtaka ya ufujaji wa pesa za umma.

Korane alikuwa ashtakiwe siku ya Jumatatu kuhusiana na madai ya ubadhirifu wa takriban shilingi milioni 233 ruzuku ya benki ya dunia lakini kesi hiyo ikaahirishwa hadi Jumanne.

Alizuiliwa katika seli za tume ya maadili na kupambana na ufiadi (EACC) mjini Nairobi.

Mkurugenzi wa mashtaka ya umma Noordin Haji siku ya Alhamisi wiki iliyopita aliagiza kushtakiwa kwa gavana huyo.

Katika taarifa yake, Haji alisema kwamba amewakabidhi ripoti ya uchunguzi maafisa wa mashtaka wenye tajiriba na kujiondoa kutoka kesi hiyo kwa sababu inahusisha kaunti anamozaliwa.

Wengine wanaokabiliwa na mashtaka ni waziri wa fedha wa kaunti hiyo Ibrahim Malow, mkuu wa hazina Mohammed Abdullahi, waziri wa manisipaa Abdi Shale na mkuu wa uhasibu Ahmed Aden.

Iligunduliwa kwamba badala ya pesa hizo kutumika kwa ujenzi wa soko, kukarabati barabara za mjini Garissa, kutengeneza njia za wanaotembea kwa miguu na kutengeneza mitaro ya kupitisha maji taka zilihamishwa kwa shughuli zingine kati ya mwezi Februari – Septemba mwaka 2019.

DPP anasema uhamisho huo ulitekelezwa na maafisa wa kaunti.

Gavana Korane analaumiwa kwa kujitwika jukumu la kusimamia fedha hizo.

Maafisa hao wa kaunti wanakabiliwa na mshtaka yakiwemo kushirikiana kutekeleza uhalifu wa kiuchumi, kupuuza sheria za usimamizi wa raslimali za ummana na ubadhirifu wa pesa za umma.

Mashtaka mengine ni kutekeleza miradi bila kufuata utaratibu hatua ambayo ni kinyume na sheria za usimamizi wa fedha za umma na matumizi mabaya ya ofisi.