Jesse Were alikataliwa na Migne, licha ya pendekezo la Kimanzi

Mkufunzi mpya wa Harambee Stars Francis Kimanzi alihojiwa  na watangazaji Toldo Kuria, Diamond Okusimba na Fred Arocho.  Swali la kwanza alilokumbana nalo lilikuwa zito. Aliambiwa kwamba kuna baadhi ya watu waliosema hajawahi fanya jambo lolote la maana kukuza soka ya Kenya.

Alisema katika taaluma yake amefanya kila juhudi kuimarisha soka ya kitaifa, 'Ni kazi gani sijafanyia Kenya? Zaidi ya miaka kumi na tano nimekuwa hapa nikihandle wachezaji, na handle clubs, na kitu ya muhimu ni wachezaji wangapi wanapitia mikononi yangu? Sijui ni nini sijafanya?'

"Nashukuru Mungu kwa kupata nafasi ya tatu kuifunza timu ya taifa. Mambo ambayo nimejifunza tangu nilipoteuliwa mkufunzi kati ya mwaka 2008-2009 ni mazuri" alisema.

Mkufunzi huyo alieleza kwamba bado alikuwa na mambo aliokuwa analenga kutimiza katika timu ya taifa Harambee Stars. Alisema kuunda kikosi thabiti cha timu ya taifa ni vigumu ikilinganishwa na kuunda kikosi cha klabu.  Aliongeza kwamba timu ya taifa ya sasa inamsingi thabiti.

Je ni nini Kimanzi alijifunza kutoka kwa Sebastien Migne?" Nilijifunza kwamba mechi za kirafiki ni muhimu mno kwa timu kwa sababu zinachezwa katika mandhari yasiokuwa na shinikizo na zinampa mkufunzi nafasi ya kujaribu wachezaji mbali mbali," alijibu.

Aliulizwa kwanini wakufunzi wa humu nchini hawapewi uhuru unaopewa wakufunzi wa kigeni? Alisema kwamba dhana hiyo inafifia na kwamba yeye na Zedekiah Otieno ni matunda ya fikra mpya.

Kimanzi alieleza kwamba ameleta wachezaji wapya katika kikosi cha taifa kutokana na umuhimu wa kuwa na wachezaji wa kutosha kila wakati. Alisema hamna nafasi ya shinikizo kutoka nje kwa uteuzi wa kikosi chake, alipoulizwa ikiwa rais wa FKF Nick Mwendwa alichangia katika uteuzi wa kikosi hicho.

Alikanusha madai kuwa huenda akapendelea wachezaji wa ilokuwa timu yake katika uteuzi wa kikosi cha taifa.

Lengo lake kuu kwa sasa ni kufuzu kwa dimba la taifa bingwa barani Afrika mwaka 2021. Alisema kwamba alitaka Jesse Were ajumuishwe katika kikosi cha Harambee Stars kwa dimba la AFCON lakini pendekezo hilo lilipuuziliwa mbali na mkufunzi Migne.