Kivumbi ndani ya "Bedroom" huku Raila akimlambisha Ruto sakafu

unnamed
unnamed
Bernard Okoth ‘Imran’ wa ODM sasa ndiye mbunge mteule wa Kibra kuchukuwa nafasi ya marehemu ndugu yake Ken Okoth.

Afisa mkuu wa uchaguzi katika eneo bunge la Kibra Beatrice Muli alitangaza matokeo rasmi ya uchaguzi huo siku ya Ijumaa asubuhi.

 Okoth aliwabwaga wagombeaji wengine 23 kwa kuzoa jumla ya kura 24, 636, alifuatwa na Macdonald Mariga wa Jubilee kwa kura 11,230, Eliud Owalo wa ANC alikuwa wa tatu kwa kura 5,275, huku KHamisi Butichi wa Ford Kenya akifunga nne bora kwa kura 260.

Akihutubia wananchi punde tu baada ya uchaguzi kutangazwa Imran aliahidi kushirikiana na wapinzani wake wote ili kuleta maendeleo katika eneo bunge la Kibra.

Imran alisema yeye ni mbunge wa kwanza wa ‘Handshake’na kuapa kuunganisha jamii zote katika eneo la Kibra bila kujali vyama vyao vya kisiasa.

“Mimi ni mtoto wa kwanza wa Handshake kati ya baba Raila Odinga na Rais Uhuru Kenyatta, ajenda yangu kuu itakuwa kuunganisha jamii zote katika eneo bunge la Kibra na kutumikia wananchi wote,” Imran alisema.

Alipongeza wanachama wa vyama vingine chini ya Handshake kwa kumuunga mkono.

Imran aliungwa mkono na wanachama wa Jubilee Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru, Maina Kamanda mbunge maalum, Spika wa Kaunti ya Nairobi Beatrice Elachi na aliyekuwa mbunge wa Dagoreti South Dennis Waweru.

 Pia aliungwa mkono na magavana Alfred Mutua wa Machakos ambaye ni kinara wa chama cha Maendeleo Chap Chap, Charity Ngilu wa Kitui ambaye pia ni kiongozi wa chama cha Narck na Kivutha Kibwana wa Makueni.