Buriani Moi: Mwili wa Moi watua Kabarak

Mwili wa rais mustaafu hayati Daniel Toroitich Arap Moi tayari umewasili katika uwanja mdogo wa ndege wa Kabarak. Ndege ya kijeshi iliyoubeba mwili huo ilitua mwendo wa saa mbili na dakika 37 asubuhi.

Mwili wa Moi ulipokelewa na maafisa jeshi na kuandaliwa gwaride ya heshima.

Moi anazikwa leo nyumbani kwake Kabarak katika kaunti ya Nakuru. Maombi ya mazishi yanaandaliwa katika shule ya msingi ya Kabarak kabla ya mwili wake kusafirishwa takriban kilomita nne hadi nyumbani kwake atakapozikwa mkabala na marehemu mkewe Lena Moi aliyefariki mwaka 2004.

Mamia ya waombolezaji walianza kumiminika katika shule ya msingi ya Kabarak kuanzia mwendo saa kumi asubuhi tayari kumpa mkono wa buriani mwenda zake rais mutaafu. Kila alipowasili alipokezwa mkate na maji.

Mazishi yake yataongozwa na idara jeshi kuashiria kwamba marehemu alikuwa amiri mkuu wa majeshi kabla ya kustaafu. Mizinga 19 ya kijeshi itapigwa kwa heshima yake.

Maombi rasmi ya kumwombea hayati Moi yaliandaliwa siku ya Jumanne katika uwanja wa kimaaifa wa Nyayo na kuhudhuria marais na viongozi kadhaa wa nchi mbali mbali.