Serikali ya India imeagiza kampuni za mitandao ya kijamii kufuta maarifa yoyote yanayotaja aina mpya ya kirusi cha Corona kilichogunduliwa India kama kirusi cha India au ‘Indian variant’’.
Wizara ya IT ilisema kuwa shirika la afya duniani liliipa aina hiyo jina B.1.617 na wala si kirusi cha India . Aidha , nchi hiyo imeathirika pakubwa na aina hiyo mpya tangu Machi na sasa inafuata Marekani kwa idadi ya Jumla ya maambukizi , zaidi ya milioni 26.
Mchipuko wa janga la Corona uliuletea mfumo wetu wa afya changamoto zake si haba lakini ulisaidia kuboresha usafi. Waziri wa afya Mutahi Kagwe anasema baadhi ya watu sasa wananawa mikono zaidi. Alidokeza pia kuwa huku kumesaidia pakubwa kupunguza magonjwa hatari ya kuendesha miongoni mwa Watoto walio chini ya miaka mitano, magonjwa ya kupumua miongoni mwa rika zote na minyoo wa tumboni miongoni mwa Watoto wa shule.
Kisumu jana ilikuwa inaongoza kwa idadi ya juu zaidi ya maambukizi ya Covid 19 ikifuatwa na Nairobi. Kati ya visa 573 vilivyosajiliwa jana , kaunti hiyo iliripoti visa 103, ikifuatwa na Nairobi iliyosajili 63. Visa hivyo vilitokana na sampuli 5,800 zilizopimwa, idadi hiyo ikiwakilisha kiwango cha juu cha maambukizi cha asilimia 9.9. Vifo sita pia viliripotiwa na wagonjwa 119 wamo ICU.
Kamati ya kitaifa ya kupambana na Covid 19 imekutaka kuhakikisha unafuata mikakati ya kukuepusha na maambukizi ya Covid 19 ili kuzidi kupunguza kiwango chetu cha maambukizi.
Jopo hilo limelaani ongezeko la visa vya baadhi Wakenya ambao wanakiuka kanuni zilizowekwa na serikali licha ya kuwepo tishio la kukabiliwa na aina ya Covid ya B.1.617 ambayo imevuruga India na vile vile imepatikana katika kaunti za Kisumu na Kilifi.