logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Mahakama yazuia serikali kuwasimamisha kazi maafisa 67 wa polisi

Mahakama iliagiza kesi hiyo kusikizwa mnamo Novemba 23 kwa maelekezo zaidi.

image
na Davis Ojiambo

Habari20 November 2023 - 14:10

Muhtasari


  • • Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei Alhamisi wiki jana alimwagiza Inspekta Jenerali wa Polisi Japhet Koome kuwasimamisha kazi maafisa hao kutokana na pendekezo la Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi.
  • • Maafisa hao walienda kortini kusimamisha agizo hilo wakitaja ukiukaji wa taratibu za kinidhamu kama ilivyoainishwa katika Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi.
Mkuu wa utumishi wa Umma Felix Koskei

Mahakama Kuu imetoa maamuzi ya kusitisha agizo la serikali la kutaka baadhi ya maafisa wa polisi 67 kusimamishwa kazi kwa madai ya kupokea hongo na makosa mengine.

Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei Alhamisi wiki jana alimwagiza Inspekta Jenerali wa Polisi Japhet Koome kuwasimamisha kazi maafisa hao kutokana na pendekezo la Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi.

Lakini maafisa hao walienda kortini kusimamisha agizo hilo wakitaja ukiukaji wa taratibu za kinidhamu kama ilivyoainishwa katika Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi.

Kupitia kwa wakili Danstan Omari, walitaka maagizo ya kusitishwa kwa agizo la Koskei wakisema lingekiuka pia haki yao ya kuchukuliwa hatua za kiutawala kwa kuwa hata hawakufahamishwa kuhusu uamuzi wa kuwasimamisha kazi.

Jaji Chacha Mwita, baada ya kusoma maombi hayo, alikubali maagizo hayo.

"Amri ya kihafidhina inatolewa kuwazuia walalamishi kutekeleza agizo lililowasilishwa kupitia barua ya Novemba 10 na mshatikwa wa kwanza kupendekeza kusimamishwa kazi kwa wahusika hadi mahakama hii itakapotoa amri nyingine," Jaji Mwita alisema katika maagizo ya Novemba 20.

EACC imeorodheshwa kama mhojiwa wa kwanza huku Koskei akiwa mjibu wa pili.

Pia walioshtakiwa ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Inspekta wa polisi, Tume ya Kitaifa ya Huduma ya Polisi, Tume ya Huduma ya Uchapishaji na Waziri wa Mambo ya Ndani miongoni mwa wengine.

Mahakama iliagiza kesi hiyo kusikizwa mnamo Novemba 23 kwa maelekezo zaidi.

Katika barua iliyoandikwa Novemba 10, afisa mkuu mtendaji wa EACC Twalib Mbarak alisema maafisa hao walikamatwa kwa kupokea hongo na utovu wa nidhamu.

“Kifungu cha 42(7) cha Sheria ya Uongozi na Uadilifu kinatamka kwamba, kwa kuzingatia Katiba na kanuni yoyote ya utekelezaji wa Maadili, Afisa wa Serikali au umma anaweza kusimamishwa kazi kusubiri uchunguzi na uamuzi wa tuhuma zinazotolewa dhidi ya afisa wa serikali au umma pale ambapo kusimamishwa kazi kunazingatiwa kuwa ni muhimu," Mbarak alisema.

Maafisa wote 67 wameorodheshwa kama wahusika.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved