logo

NOW ON AIR

Listen in Live

Rigathi Gachagua afunguka kuhusu ugonjwa uliompelekea kulazwa wakati maseneta wakimuondoa ofisini

Gachagua amezungumza kwa mara ya kwanza hadharani tangu maseneta wamuondoe ofisini siku ya Alhamisi.

image
na SAMUEL MAINAjournalist

Habari20 October 2024 - 14:54

Muhtasari


  • Huku akiwahutubia wanahabari nje ya Hospitali ya Karen , Gachagua alithibitisha kuwa kweli aliugua baada ya seneti kuchukua mapumziko ya mchana siku ya Alhamisi.
  • "Baada ya kupata utulivu, daktari aliniambia kuwa kama ningechelewa kwa dakika 20, tungezungumza hadithi nyingine leo," alisema.

Naibu rais aliyetimuliwa Geoffrey Rigathi Gachagua amezungumza kwa mara ya kwanza hadharani tangu maseneta wamuondoe ofisini siku ya Alhamisi.

Huku akiwahutubia wanahabari nje ya Hospitali ya Karen mnamo Jumapili, Oktoba 20, 2024, Gachagua alithibitisha kuwa kweli aliugua baada ya seneti kuchukua mapumziko ya mchana siku ya Alhamisi.

Gachagua alisema kuwa baada ya seneti kwenda mapumziko, alikwenda kula chakula cha mchana pamoja na mawakili wake na viongozi wengine kabla ya kuamua kupita ofisini kwake kuchukua karatasi alizohitaji. Anasema kuwa alipokuwa akielekea ofisini kwake ndipo alianza kusikia maumivu kifuani.

"Wakati nilikuwa naenda ofisini ghafla nilipata maumivu makali sana kwenye kifua. Nilikaa chini na maumivu yakaendelea, yalikuwa makali sana na makali sana,” Rigathi Gachagua alisema.

Aliendelea, “Nilimpigia simu daktari wangu Dkt. Gikonyo wa hospitali hii ambaye amekuwa daktari wangu kwa miaka 20 iliyopita na nilimweleza kwa ufupi jinsi nilivyokuwa nikihisi. Aliniuliza kuhusu ukali wa maumivu nikamwambia ni makali sana. Tukiwa tunaongea nilianza kukosa pumzi.  Dkt. Gikonyo aliniagiza kuacha kila kitu nilichokuwa nikifanya na kufika hapa kwa Karen haraka iwezekanavyo. Aliniambia nilichokieleza si kitu kizuri, na ni lazima nije hapa.”

Naibu rais huyo aliyetimuliwa anasema kwamba aliheshimu maagizo ya daktari mara moja na akakimbizwa katika Hospitali ya Karen na timu yake.

Anaongeza kuwa madaktari katika Hospitali ya Karen walifanikiwa kumtuliza lakini akabainisha kuwa walionya kwamba ingekuwa mbaya zaidi ikiwa hangefika hospitalini kwa wakati.

"Baada ya kupata utulivu, daktari aliniambia kuwa kama ningechelewa kwa dakika 20, tungezungumza hadithi nyingine leo," alisema.

Naibu rais aliyetimuliwa alisema kuwa ingawa hajapona kabisa, sasa anahisi vizuri na yuko nje ya hatari.

"Maumivu makali yamepita. Kilichopo kinaweza kudhibitiwa kwa mwanaume. Mwanaume lazima awe na uwezo wa kustahimili baadhi ya mambo haya madogo. Katika tathmini yake (daktari), niko nje ya hatari. Lakini nilipokuja ilikuwa kali sana,” alisema.


RADIO JAMBO FREQUENCIES

Kisumu 100.1 | Mombasa 92.3 | Nakuru 96.9 | Eldoret 99.5 | Nyeri 99.3 | Nyahururu 97.3 | Webuye 95.3 | Meru 92.7 | Kitui 104.9 | Kibwezi 104.7 | Voi 105.7 | Malindi 98.1 | Lamu 104.7 | Narok 97.3 | Kapenguria 99.7 | Kisii 89.3 | Garissa 104.3 | Maralal 97.3 | Lodwar 92.7


logo© Radio Jambo 2024. All rights reserved